Thursday, August 16, 2012

Kuporomoka kwa uchumi wa dunia na mikakati ya Tanzania kujikwamua kiuchumi


Mwenyekiti Wa Cuf Taifa-Prof Ibrahim Haruna Lipumba

Uchumi wa nchi muhimu zilizoendelea ikiwemo Marekani, Jumuia ya Ulaya na Japan bado unayumba miaka minne baada ya mtikisiko mkubwa wa uchumi mwaka 2008. Mtikisiko huo ulisababishwa na sera mbovu ya usimamizi wa sekta ya fedha ilioruhusu mfumko wa bei za nyumba na uwekezaji mkubwa katika sekta hiyo. Tufe la mfumko wa bei za nyumba lilipopasuka na bei hizo kuporomoka, mabenki mengi yalikabiliwa na tatizo la kufilisika kwa sababu mikopo yao katika sekta ya nyumba haikuweza kulipika na amana zilizohusiana na sekta ya nyumba ziliporomoka. Familia nyingi zilikopa kwa kutumia thamani ya nyumba zao kama dhamana. Kuporomoka kwa bei za nyumba ziliondoa uwezo wa kukopa na kuwalazimisha walipe madeni yao na kwa hiyo kupunguza matumizi ya kununua bidhaa na huduma. Familia zinapopunguza matumizi ya kawaida makampuni yanayotengeneza bidhaa na kutoa huduma yanakosa soko na kulazimika kupunguza uzalishaji wa bidhaa na huduma na kupunguza wafanyakazi. Watu wa kikosa ajira wanapunguza matumizi na hivyo kuathiri uzalishaji wa bidhaa na huduma na kuchochea uachishwaji wa kazi wa watu wengi zaidi. Makampuni yanayoshindwa kuuza bidhaa zao yanapunguza wafanyakazi na yanaacha kuwekeza vitega uchumi kupanua shughuli zao kwa ukosefu wa soko la bidhaa na huduma zao. Kupunguza uwekezaji kunaongeza ukosefu wa ajira.
Mahitaji ya soko la bidhaa na huduma yanapopungua, Benki Kuu inaweza kusaidia kuongeza mahitaji hayo kwa kupunguza riba. Riba inapopungua gharama za mikopo inakuwa rahisi na kwa hiyo familia na wawekezaji wanaweza kukopa. Katika mtikisiko wa uchumi ulioanza mwaka 2008, riba za Benki Kuu zimepunguzwa mpaka kufikia karibu ya sufuri na kwa hiyo haziwezi kupunguzwa zaidi ya hapo. Uwezo wa sera za riba kusaidia kuongeza matumizi ya sekta binafsi na kaya umetoweka kwa sababu riba za Benki Kuu haziwezi kwenda chini ya sufuri. Zaidi ya hapo ikiwa makampuni hayana imani kuwa kutakuwa na ongezeko la mahitaji ya bidhaa zao, hawewezi kuongeza uwekezaji hata kama riba ni za chini.
Benki Kuu inaweza kuongeza matumizi ya kaya na sekta binafsi ikiwa itaonyesha kuwa sera zake zitaongeza mfumko wa bei. Ikiwa mfumko wa bei ni wa juu, akiba ya fedha taslimu inapungua thamani yake. Watu watabaini kuwa vyema kununua bidhaa za kudumu kuliko kuweka akiba ya pesa taslimu. Wachumi wengi wamependekeza sera hii ya kuongeza mfumko wa bei kutoka asilimia 2 na kufikia asilimia 4. Hata hivyo Benki Kuu nyingi za nchi zilizoendelea zinaongozwa na mahifidhina wanaoamini kuwa jukumu lao kubwa ni kuhakikisha mfumko wa bei hauzidi asilimia 2. Hawaikubali kabisa sera itakayoongeza mfumko wa bei kwa muda ili kuhamasisha sekta binafsi inunue bidhaa na huduma badala ya kuweka akiba.
Katika hali ya ukosefu wa soko la kuuza bidhaa na huduma kila kampuni inafanya uamuzi wa busara wa kupunguza matumizi na uwekezaji. Familia zinazokabiliwa na kupungua kwa utajiri walionao na kuongezeka kwa madeni wanaamua kupunguza matumizi na kuongeza akiba. Uamuzi wa familia moja moja na kampuni moja moja una mantiki lakini kwa pamoja kila familia na kampuni zikipunguza matumizi pato lao la pamoja linapungua kwani matumizi yako ndiyo mapato ya mwingine. Ili kukabiliana na tatizo hili serikali ya nchi zilizoendelea zinawajibu wa kuongeza matumizi kuziba pengo lililoachwa na sekta binafsi. Serikali inaweza kuongeza matumizi kwa kuongeza nakisi ya bajeti. Sekta binafsi inapokuwa na kipato kidogo, mapato ya serikali ambayo yanatokana na kodi yanapungua. Kuongeza matumizi wakati mapato yanapungua maana yake ni kuongeza nakisi ya bajeti na kwa hiyo kuongeza deni la serikali. Sera ya kuongeza matumizi ya serikali na nakisi ya bajeti ni ya muda mfupi.Uchumi ukiimarika serikali itakusanya kodi nyingi na pia ina fursa ya kupunguza matumizi na kwa hiyo kuwa na ziada katika bajeti yake na kupunguza deni lake.
Sera za kuongeza matumizi ya serikali na hivyo kuwa na nakisi ya bajeti kubwa na kuongeza deni la serikali imepingwa na wahafidhina. Nchini Marekani Chama cha Republican ambacho kina Wawakilishi wengi katika Baraza la Wawakilishi kinapinga kuongeza matumizi ya serikali kwa madai kuwa itaongeza nakisi na kuongeza deni la taifa. Sera za nchi za Jumuiya za Ulaya, kanda ya euro zinaongozwa na fikra za Serikali ya Ujerumani ambayo inapinga serikali kuwa na nakisi kubwa ya bajeti. Nchi wanachama wa kanda ya euro hawana Benki Kuu zao zilizo huru na hawana sarafu zao wenyewe. Hawana uwezo wa kuongeza nakisi ya bajeti zao bila kuongeza riba. Serikali za nchi za Ulaya Kusini – Hispania, Italia, Ureno na Ireland wanalipa riba kubwa sana wanapokopa katika masoko ya fedha. Uingereza ambayo nakisi yake ya bajeti ni kubwa zaidi ya Hispania inatozwa riba ndogo kwa sababu ina Benki Kuu na  sarafu yake yenyewe na kwa hiyo ina uwezo wa kulipa madeni yake kwa kuchapisha fedha zake kwa wingi.
Hatua za mwanzo za kukabiliana na mtikisiko wa uchumi mwaka 2008 ulikuwa sahihi. Nchi nyingi ziliongeza matumizi ya serikali. Kwa sababu ya itikadi za kihafidhina, kuongezeka kwa nakisi ya bajeti na kukua kwa deni la taifa likaleta mabadiliko ya sera serikali zikaanza kubana matumizi kabla ya uchumi kutengamaa na sekta binafsi kuimarika. Sera sahihi ni kuendelea kuongeza matumizi ya serikali katika kipindi cha muda mfupi na kuweka mpango wa kukabiliana na nakisi ya bajeti na deni la serikali kwa muda wa kati baada ya sekta binafsi kuimarika na hivyo kuongeza ajira na kodi za serikali. Misamaha ya kodi kwa matajiri iondolewe wakati wananchi wenye kipato cha chini na cha kati waendelee kunufaika na misamaha ya kodi katika kipindi cha muda mfupi mpaka uchumi utakapoimarika.
Baada ya mgogoro wa fedha duniani wa mwaka 2008, jumla la pato la dunia lilianguka kwa asilimia 0.6 mwaka 2009. Uchumi wa nchi zilizoendelea ndiyo ulioanguka zaidi. Pato la taifa la Ujerumani lilianguka kwa asilimia 5.1, Japan na Italia kwa asilimia 5.5, Uingereza asilimia 4.4 na Marekani kwa asilimia 3.5. China haikuathirika sana na mtikisiko wa uchumi wa dunia kwa sababu ya hatua zilizochukuliwa na serikali ya China za kuongeza matumizi kukabiliana na kupungua kwa mahitaji katika soko la bidhaa. Kasi ya kukua kwa pato la taifa la China ulipungua kutoka asilimia 14.2 mwaka 2007 na kufikia asilimia 9.2. Juhudi za pamoja za  kufufua uchumi za Marekani, nchi za Jumuiya ya Ulaya na nchi zinazoendelea hasa Uchina, India na Brazil zilisaidia kuongeza ukuaji wa uchumi wa dunia na kufikia asilimia 5.3 mwaka 2010. Lakini kupunguza kwa matumizi ya serikali na mgogoro wa Euro umepunguza ukuaji wa uchumi na kufikia asilimia 3.9 mwaka 2011 na makadirio ya 3.5 mwaka 2012.
Nchi za Jumuiya ya Ulaya zinakabiliwa na mdororo mwingine wa uchumi kwa sababu ya matatizo ya Euro. Pato la kanda ya Euro linakadiriwa kupungua kwa asilimia 0.3 mwaka 2012. Nchi za Ulaya ya Kusini – Ugiriki, Hispania, Italia na Ureno ndizo zimeathirika zaidi kwa kuporomoka kwa uchumi na kuongezeka kwa ukosefu wa ajira. Pato la taifa la Marekani litakua kidogo tu kwa asilimia 2.1. Ukosefu wa ajira unabakia juu sana zaidi ya asilimia 8.0.
Inasikitisha kuwa nchi zilizoendelea zimekumbwa na itikadi ya kihafidhina na wameshindwa kufuata ushauri wa wachumi wa kimataifa wa kuongeza matumizi ya serikali katika kipindi cha muda mfupi na kushughulikia nakisi ya bajeti na ukuaji wa deni la taifa katika kipindi cha muda wa kati. Kususua kwa uchumi wa nchi zilizoendelea kunaongeza matatizo kwa nchi maskini katika mikakati yao ya kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuutokomeza umaskini. Nchi maskini kama Tanzania inategemea soko la nchi zilizoendelea kuuza bidhaa zake, wengi wa watalii wanaokuja Tanzania wanatoka nchi za Ulaya, Wawekezaji wa vitega uchumi wanatoka nchi zilizoendelea na serikali inategemea misaada na mikopo toka nchi hizo.
Kati karne ya 21 nguvu za uchumi za mataifa umeanza kubadilika. Uwezo wa kiuchumi wa nchi za magharibi unapungua ukilinganisha na nchi za Asia. Nchi nyingi zinazoendelea na hasa China zimeendelea kukuza uchumi wao pamoja na kuathiriwa na mtikisiko wa uchumi wa nchi zilizoendelea. Nchi yetu inabidi iweke mkakati wa kushirikiana na nchi zinazoibuka na kuwa na nguvu za kiuchumi kwa manufaa ya nchi yetu lakini tusigezwe kuwa soko la bidhaa duni toka nchi hizo.
Kwa kuwa nchi yetu iko nyuma katika maendeleo ya uchumi, tuna fursa nyingi za kutumia elimu, utaalamu na teknolojia ambayo imeishagunduliwa ili tukuze pato letu la taifa, tuongeza ajira yenye kipato kizuri, na hatua kwa hatua tuotokomeza umaskini. Ni muhimu kwa Watanzania tujihamasishe na tuwe na motisha wa kujifunza na kutumia teknolojia iliyopo tukizingatia mazingira tuliyonayo. Kuna fursa kubwa ya kuongeza uzalishaji na tija kwa kutumia teknolojia bora katika sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu, madini, nishati, viwanda, usafiri na mawasiliano, na huduma za jamii.
Kuwepo kwa fursa za kukuza uchumi katika sekta mbalimbali hakuna maana kuwa fursa hizo zinaweza kutumiwa kirahisi. Kuwa na uchumi wa soko na utengamano wa uchumi mpana (macroeconomic stability), fedha za kigeni kupatikana kwa bei ya soko na kuondoa vikwazo vya biashara ya nje hakutoshi kuiwezesha nchi kukua kwa asilimia 8-10 kwa muda wa miaka 20-30 na kuubadilisha mfumo wa uchumi wake kutoka kutegemea kilimo na sekta isiyo rasmi na kuongeza ajira katika sekta ya viwanda na huduma za kisasa.  Kukua kwa uchumi kwa kasi hiyo kunahitajika ili kuhakikisha tunautokomeza umaskini.
Tunahitaji sera za maksudi za kuasisi maendeleo makubwa ya viwanda kwa kuanzia na viwanda vinavyotumia malighafi inayozalishwa nchini. Kuanzisha na kuendeleza viwanda hakutafanikiwa kwa kuachia mfumo wa soko peke yake uamue maeneo ya uwekezaji. Juhudi maalum ya serikali na nidhamu ya hali ya juu ya utekelezaji inahitajika. Serikali inapaswa kutambua vikwazo vinavyokwamisha maendeleo ya viwanda na kuviondoa. Miundombinu ya usafiri na umeme ni muhimu kwa maendeleo ya kasi ya viwanda na uchumi kwa ujumla. Pamoja na kuelewa kuwepo kwa tatizo hili kwa muda mrefu, inasikitisha kuwa serikali imeshindwa kabisa kutekekeleza mipango yakutatua matatizo ya miundombinu. Serikali imeshindwa kuweka vipaumbele na kutekeleza miradi michache ikakamilika kabla ya kuanza miradi mingine.
Serikali imekuwa na mipango mingi isiyo tekelezwa au kutekelezeka. Kuna Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025 ambayo inalenga kuwa Tanzania iwe ni nchi yenye kiwango cha kati cha mapato (middle income country) na hali bora ya maisha kwa wananchi. Mpango Maalum wa Kuharakisha Maendeleo ya Tanzania (Tanzania Mini Tiger Plan 2020) ambao haijulikani umeishia wapi.  Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania – MKUKUTA I na MKUKUTA II na Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano 2010-15. MKUKUTA I na MKUKUTA II hazikufanyiwa makadirio ya gharama za utekelezaji wake. Gharama za mpango wa miaka mitano ni kubwa mno na serikali haina fedha ya kuugharamia.
Pamoja na matatizo ya uchumi wa dunia, Tanzania inaweza ikatumia fursa ya kuwa nyuma na kutumia teknolojia iliyopo kukuza uchumi wake. Watanzania tunahitaji tutafakari hali halisi tuliyonayo na tubuni sera na mikakati ya pamoja inayotekelezeka ili tujikwamue toka dimbwi la umaskini. Misingi muhimu ya sera na mikakati hiyo iwe kuitumia vizuri mali ya asili ya Tanzania kwa manufaa ya wananchi wote huku tukilinda mazingira yetu. Kuwekeza kwenye afya ya watoto wa Tanzania toka wakiwa katika mimba za mama zao kwa kuhakikisha kina mama wajawazito na watoto wachanga wanapata lishe bora. Kuwekeza katika elimu ya watoto wa Tanzania toka shule za chekechea na kuendelea. Kuweka msisitizo maalum katika elimu ya hesabu, sayansi na teknolojia. Kuwekeza katika kilimo hasa cha chakula kama vile mahindi, mpunga, maharage, jamii ya kunde na mbegu za mafuta kukidhi mahitaji ya ndani na kuuza masoko ya nje hasa nchi za jirani. Kuwekeza katika miundombinu ya barabara, umeme, maji na mawasiliano. Kuweka mkakati madhubuti wa kuanzisha na kuendeleza viwanda vinavyotumia malighafi ya ndani na kuajiri watu wengi kama vile viwanda vya nguo na mavazi, viatu na bidhaa za ngozi, vifaa vya matumizi ya nyumbani na vifaa vya umeme na elektroniki.
Kubuni na kutekeleza mikakati hii Tanzania inahitaji uongozi wenye dira utakaowaunganisha na kuwahamasisha Watanzania tujielimishe na tutumie raslimali na mali ya asili ya nchi yetu kuwaletea neema wananchi wote.

No comments:

Post a Comment