Saturday, August 25, 2012

MUDA WA KULITEKA JANGWA UMEWADIA.

Mh Abdul Kambaya-
Naibu Mkurugenzi wa Habari,
Mahusiano na Haki za Binadamu
wa Chama cha Wananchi (CUF)
KATIKA KUJIANDAA NA SAFARI YA KUELEKEA ARUSHA TUTALIKABILI JANGWA TAREHE 09-09-2012
CUF-Chama Cha Wananchi, kinawatangazia Mkutano Mkubwa wa Hadhara utaofanyika siku ya Jumapili kwa tarehe tajwa hapo juu.
Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na Viongozi wote wa Kitaifa wa CUF. Mkutano utaanza saa nne asubuhi mpaka saa kumi na mbili jioni. Profesa Ibrahim Lipumba atawaoongoza Wanachama wa CUF katik

a Mkakati mdogo Ujulikanao kwa jina la MCHAKA MCHAKA MPAKA 2015 kuzunguka Mikoa sita kukutana na Watanzania ili kuweza kujadili muelekeo wa Nchi yetu na hatima ya Watanzania chini ya siasa Uchwara za Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Kila Mwanacuf unaesoma taarif a hii, tafadhali mjulishe na mwenzio. Makabwela na Walala hoi wote tafadhalini ASIBAKI MTU NYUMBANI . Mabepari wamefanya Mkutano wao na mmewashuhudia, sasa ni zamu ya MAKABWELA NA WALALA HOI kukumbuka historia ya mababu zetu ndani ya Jangwa la MAKABWELA. MCHAKA MCHAKA MPAKA 2015

Thursday, August 23, 2012

KUPANDA KWA BEI YA CHAKULA KATIKA SOKO LA DUNIA KUWE CHACHU YA KUASISI MAPINDUZI YA KILIMO TANZANIA


Prof Ibrahim Haruna Lupumba-Mwenyekiti Wa Cuf Taifa.
Mwanzono mwa mwezi wa Agosti nilienda Tabora kumtazama na kumpa pole shangazi yangu anayeumwa. Hali ya bei ya chakula hasa mahindi ilinitisha. Kwa kawaida mwezi wa Agosti ni baada ya mavuno. Bei ya mahindi huwa bado iko chini. Debe la mahindi huwa halizidi shilingi 5000/- Mwaka huu agosti mwanzoni bei ya debe la mahindi ni shilingi 10000/-. Ifikapa Disemba bei ya mahindi inaweza kuruka na kufikia shilingi 15000/- au zaidi.
Tathmini ya serikali kama ilivyoelezwa na Waziri wa Kilimo na Ushirika katika hotuba yake ya bajeti kuwa “ Matokeo ya tathmini ya awali ya hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula na utabiri wa hali ya chakula kwa mwaka 2012/2013 yanaonesha kwamba uzalishaji wa mazao ya chakula utafikia tani 13,572,804 ikilinganishwa na mahitaji ya chakula yanayokadiriwa kuwa tani 11,990,115 kwa mwaka 2012/2013. Taifa linatarajia kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 113 na hivyo kuwa na ziada ya tani 1,582,690. Tathmini hiyo ilibaini kuwepo na ziada ya chakula katika mikoa nane (8) ya Iringa, Rukwa, Mbeya, Kagera, Mtwara, Kigoma, Ruvuma na Morogoro; utoshelevu katika mikoa saba (7) ya Pwani, Mara, Tanga, Lindi, Mwanza, Singida na Dodoma; na uhaba katika mikoa sita (6) ya Shinyanga, Tabora, Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Dar es Salaam”
 Hali ya bei ya vyakula katika maeneo mengi ya nchi haionyeshi kuwepo kwa ziada kubwa. Vile vile hali ya biashara ya mazao ya vyakula ndani ya mipaka ya Tanzania ina vikwazo. Maeneo yenye ziada hayauzi chakula cha kutosha kwenye maeneo yenye upungufu. Bei ya mahindi  Tabora ingekuwa ya chini kama wafanyabiashara wangenunua mahindi toka Mpanda mkoa wa Rukwa na kuyauza Tabora.
Hata katika miaka ambayo chakula kilichozalishwa nchini kinaonekana kukidhi mahitaji ya taifa, ukosefu wa lishe bora ni tatizo la muda mrefu. Miaka 50 baada ya uhuru, theluthi moja  ya Watanzania ikimaanisha Mtanzania mmoja katika kila Watanzania watatu hawana lishe bora. Asilimia 44 ya watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wana utapiamlo, ni wafupi kuliko wanavyostaili kuwa kwa sababu ya kukosa chakula cha kutosha na lishe bora. Watoto wasiokuwa na lishe bora wanashindwa kujenga kinga ya mwili, maungo yao siyo imara na hawajengi ubongo wao vizuri na kwa hiyo wanakuwa wagumu  kujifunza na kufundishwa. Kuhakikisha kuwa kina mama wajawazito na watoto wote wanapata lishe bora ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele na familia, jamii na serikali kwa ujumla.
Hali ya bei ya mazao ya nafaka  hasa mahindi katika soko la dunia  inatisha. Tathmini ya Waziri wa Kilimo katika hotuba yake ya bajeti imepitwa na wakati kwani alieleza kuwa  taarifa ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (Food and Agriculture Organisation - FAO) iliyotolewa mwezi Juni 2012, inaonesha kuwa katika mwaka 2011/2012, uzalishaji wa nafaka duniani unatazamiwa kuongezeka kwa asilimia 3.2. Jumla ya tani  bilioni 2.42 za nafaka zitazalishwa ikilinganishwa na matumizi ya nafaka ya tani bilioni 2.38 kwa mwaka 2012/2013, matumizi ya nafaka kwa ajili ya chakula cha mifugo yataongezeka kwa asilimia 3.8 wakati matumizi ya chakula yanatazamiwa kuongezeka kwa asilimia moja (1). Akiba ya nafaka duniani inatazamiwa kuongezeka kwa tani milioni 36 na kufikia tani milioni 548 sawa na ongezeko la asilimia saba (7) kutoka kiwango cha mwaka jana.”
Marekani ya Magharibi ya Kati ndiyo eneo linalozalisha mahindi kwa wingi. Mwezi wa julai mwaka huu ulikuwa na joto kali katika eneo hili kuliko miaka yote 117 iliyopita tangu kumbukumbu za hali ya joto kuanza kutunzwa. Marekani kwa ujumla imekumbwa na ukame mbaya kupita yote kwa muda wa miaka 50. Marekani ndiyo inayoongoza katika kuzalisha na kuuza nafaka katika soko la dunia. Kwa sababu ya ukame uzalishaji wa mahindi na maharage ya soya utapungua sana mwaka huu na tayari bei za mahindi na soya zimevunja rekodi ya bei ya mwaka 2008.
Nchini Marekani na Ulaya mahindi yanatumika sana kama chakula cha mifugo. Mexico, nchi za Marekani ya kati na Afrika, mahindi ni chakula muhimu cha binadamu. Nchini Marekani ng’ombe analishwa kilo 30 za mahindi ili kupata kilo moja ya nyama.
Wamarekani pia wanatumia mahindi kutengeneza ethanol inayotumiwa kama petroli mbadala. Katika kila majunia 100 ya mahindi yanayozalishwa Marekani, 40 yanatumiwa kutengeneza ethanol. Mahindi yanayotumiwa kutengeneza ethanol kujaza tenki la gari ya familia ya Marekani yanatosha ugali wa mwaka mzima wa mkulima wa Tabora. Utumiaji wa mahindi kutengeneza ethanol kunaongeza bei ya mahindi katika soko la dunia.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa – FAO, Jose Graziano da Silva ameiomba Marekani kusitisha mara moja utumiaji wa mahindi kutengeneza ethanol ili kupunguza mfumko wa bei ya mahindi katika soko la dunia. Katika mwaka wa uchaguzi mkuu, Serikali ya Marekani haielekei kukubali wito wa Jumiya ya Kimataifa ya kusitisha matumizi ya mahindi kutengeneza ethanol kwa sababu wakulima wa mahindi wa Marekani ya magharibi ya kati wanaipenda sera ya kutumia mahindi kutengeneza ethanol kwa kuwa inaongeza bei ya mahindi. Majimbo yenye wakulima wa mahindi kama vile Iowa ni muhimu katika mkakati wa Rais Obama na chama cha Democrats kushinda uchaguzi Novemba 2012.
Kupanda kwa bei ya chakula duniani ni changamoto na fursa. Bei  ya chakula katika soko la dunia itaendelea kuwa juu kwa muda mrefu kwa sababu ya mahitaji ya nafaka kulisha mifugo na matumizi ya mazao kutengeneza petroli mbadala.
Kilimo chetu kimeendelea kuwa duni kwa sababu zisizokuwa na msingi. Tuna ardhi ya kutosha, mito na maziwa makubwa. Jiografia ya Tanzania inafanya nchi yetu iwe na majimbo yenye hali ya hewa tofauti. Mazao mbali mbali ya chakula na biashara yanastawi katika ardhi ya Tanzania, nchi yetu ina uwezo mkubwa wa kuzalisha mazao ya chakula na biashara kukidhi mahitaji ya ndani na kuuza nchi za nje. Lakini miaka 50 baada ya Uhuru, Tanzania haijitoshelezi kwa chakula kwa sababu ya sera na uongozi usiokuwa na dira sahihi ya maendeleo.
 Nchi yetu ina ardhi kubwa inayokubali aina mbambali ya mazao. Tunatumiai robo tu ya ardhi yote inayofaa kwa kilimo. Ardhi inayolimwa haipandwi mbegu bora. Kati ya wakulima 100 wa Tanzania, 90 wanatumia mbegu za kienyeji zisizokuwa na uwezo wa uzalishaji mkubwa. Wakulima wengi hawatumii mbolea. Mfumo wa usambazaji wa mbegu bora, mbolea na pembejeo nyingine ni hafifu sana. Utaratibu wa mikopo kwa wakulima wakununulia zana na pembejeo haupo. Chini ya asilimia 1 ya ardhi inayofaa kilimo cha umwagiliaji imeendelezwa na kutumiwa. Maeneo yenye mfumo wa umwagiliaji  hayatunzwi na kukarabatiwa na kwa hiyo hayazalishi kwa uwezo wake. Matumizi ya matrekta katika kilimo bado ni madogo sana. Kwa mfano mkoa wa Kigoma wenye ardhi kubwa, mabonde yenye rutuba mito na vijito vingi ina matrekta makubwa 25 na matrekta ya mkono 176 tu.
Tanzania imekosa sera sahihi ya kukuza kilimo na kuinua hali za maisha ya wakulima. Zana za kilimo na pembejeo haziwafikii wakulima na hata zinapowafikia huwa zimechelewa na kufika nje ya wakati. Pamoja na serikali kudai kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wetu, kilimo hakipewi kipaumbele. Tangu tupate uhuru wa taifa letu matumizi halisi ya sekta ya kilimo ya kila mwaka hayajawahi kuzidi asilimia tano ya bajeti yote ya Serikali. Nchi yetu haina huduma bora kwa ajili ya kukuza kilimo cha kisasa na kwa ujumla kumekuwa na udhaifu mkubwa hasa katika maeneo ya uwekezaji kwenye tafiti, motisha kwa wakulima ili wajaribu mambo mapya, ushauri na utaalamu kwa wakulima, mikopo ya zana za kilimo na pembejeo, barabara na mawasiliano vijijini.
Hatua za muda mfupi za kukabiliana na ongezeko kubwa la bei katika baadhi ya wilaya za Tanzania ni kuruhusu na kurahisisha biashara ya ndani ya mazao ya chakula. Serikali irahisishe mfumo wa kodi na ushuru wa mazao ya kilimo; ikiwa ni pamoja na kufuta ushuru na ada zote za mazao katika ngazi ya mkulima ili kuongeza motisha kwa wananchi kuwekeza juhudi zaidi katika uzalishaji wa mazao ya kilimo. Vizuizi vyote visivyo na msingi katika biashara ya mazao yote ndani ya nchi viondolewe.
Wafanyabiashara wa ndani wapewe motisha wa kuwekeza katika ununuzi wa nafaka toka maeneo yenye ziada na kuuza kwenye maeneo yenye upungufu. Sera za serikali katika mazao ya chakula hazitabiriki. Wakuu wa Wilaya wanaweza kuzuia uuzaji wa nafaka nje ya wilaya zao. Matokeo yake hakuna wafanyabiashara wa nafaka inayozalishwa nchini wenye mtazamo wa muda mrefu badala yake kuna walanguzi wenye mtazamo wa muda mfupi.
Hivi sasa serikali ianze uhamasishaji wa uzalishaji wa mazao yanayokomaa kwa muda mfupi katika maeneo yanayopata mvua za vuli. Utaratibu mzuri wa usambazaji wa mbegu bora, mbolea na pembejeo unahitajika. Usambazaji wa vocha za mbolea umejaa ufisadi. Mbolea inachakachuliwa na haikidhi viwango na kuwapa hasara wakulima.
Wakuu wengi wa wilaya wameteuliwa kwa upendeleo wa kisiasa na hisia binafsi na hawana uwezo wa kusimamia maendeleo ya kilimo. Badala yake Wakuu wa wilaya ni vikwazo vya maendeleo ya kilimo. Wanatoa maagizo na amri zinazowakwaza wakulima. Uteuzi wa Wakuu wa wilaya na wa mikoa uzingatie uwezo wa kuongoza na kusimamia maendeleo ya kilimo.
 Sera ya Kilimo Kwanza imejikita katika kuwatumia wakulima wakubwa kuwaendeleza wakulima wadogo wadogo. Hii ni ndoto ya Alnacha. Wakulima wakubwa wanahitaji ardhi na vibarua. Maslahi ya wakulima wakubwa yanakinzana na maslahi ya wakulima wadogo wadogo. Kwa kuwa tuna ardhi ya kutosha wakulima wakubwa wenye mitaji wana nafasi katika kukuza kilimo cha Tanzania lakini wasitegemewe kuwa ndiyo chachu ya kuwaendeleza wakulima wadogo wadogo. Sera muafaka kwa Tanzania ni kuhakikisha kuwa wakulima wadogo wadogo wanashiriki katika kilimo cha biashara cha kuzalisha mazao ya ziada na kuyauza kwenye soko. Mafunzo kwa wakulima na huduma za ugani kuhusu kilimo cha kisasa ni muhimu sana. Taaluma ya ubwana na ubibi shamba irejeshewe hadhi yake na wataalam wa kilimo wapewe motisha ya kufanya kazi yao. Wakulima wapate pembejeo ikiwa ni pamoja na mbegu bora na mbolea, na zana za kilimo.
Ile ahadi ya serikali za nchi za nchi za SADC ya kutumia alau asilimia 10 ya bajeti ya serikali katika sekta ya kilimo itekelezwe. Maeneo muhimu ya kuwekeza ni pamoja na utafiti wa kilimo, barabara za vijijini na mawasiliano, mfumo wa kilimo cha umwagiliaji maji, usambazaji wa pembejeo, huduma za fedha za kuweka akiba na kukopa kununulia pembejeo.
Tanzania ina fursa ya kukuza sekta ya kilimo kwa wastani wa asilimia 8 kwa mwaka kwa muda ya miaka 10 ijayo ukilinganisha na ukuaji wa wastani wa asilimia 4 katika miaka 10 iliyopita . Tuna ardhi ya kutosha kukidhi mahitaji yetu ya chakula na kuuza nchi za nje. Sekta ya kilimo inapokua kwa kasi inachochea ukuaji wa sekta nyingine. Upatikanaji wa chakula kwa bei nafuu unapunguza gharama za maisha na gharama za kuajiri wafanyakazi wenye afya njema. Kilimo cha kisasa kinahitaji mbolea, mbegu bora na utaalamu. Gesi iliyonguduliwa inaweza kutumiwa kutengeneza mbolea. Kilimo kinahitaji huduma za usafiri – kusafirisha pembejeo na mazao ambao unaongeza ajira. Mazao ya kilimo ni malighafi katika viwanda vya kusindika nafaka, matunda, maziwa na nyama. Viwanda vya nguo na bidhaa za ngozi vinatumia malighafi inayozalishwa na kilimo. Kipato cha wakulima kinapoongezeka wananunua bidhaa za viwandani kama vile nguo, vyombo vya nyumbani, samani, mabati, saruji na vifaa vinginevyo. Mapinduzi ya kilimo yatachochea ukuaji wa sekta ya viwanda na kuongeza ajira katika sekta rasmi.
Ili kuasisi mapinduzi endelevu ya kilimo yatakayomsaidia mkulima wa kawaida Tanzania inahitaji uongozi wenye dira. Serikali ya CCM imewasaliti wakulima wa Tanzania na kuwaongezea umaskini. Jukumu muhimu la wanaharakati wa dira ya mabadiliko ni kuwaelimisha na kuwahamasisha wakulima washiriki kikamilifu katika mabadiliko ya kisiasa yatakayoasisi mapinduzi ya kilimo yatakayowanufaisha Watanzania wote.







Friday, August 17, 2012

TANZANIA INAHITAJI UONGOZI WENYE DIRA NA SERIKALI MADHUBUTI ILI KUJINASUA TOKA DIMBWI LA UMASKINI

Mwenyekiti Wa Cuf Taifa-Prof Ibrahim Lipumba

Nchi ambazo zimefanikiwa kukuza uchumi kwa kasi ya juu na kuwa na maendeleo kwa muda mrefu zimefanya hivyo kwa kuwa na uongozi adilifu, wenye dira na ulio imara katika uamuzi, utekelezaji na kujifunza toka kwenye makosa waliofanya na kujirekebisha.Kuzungumzia uongozi na uadilifu katika siasa si jambo jepesi. Hisia na mitazamo ya watu wa kawaida kuhusiana na ‘siasa’ imekuwa ya kuihusisha fani hiyo na tamaa, ubinafsi, uroho, unafiki, ulaghai, upotovu, uovu, fitina, hiyana, na hata hujuma. Tena si watu wa kawaida tu bali hata baadhi ya wasomi wetu wanaonekana kuiona hivyo. Kwa wananchi wetu wa kawaida mtu akisifiwa kuwa huyo kwa siasa humuwezi, maana yake ni gwiji wa uongo na laghai. Hali hiyo kwa kiasi kikubwa imesababishwa na ubabaishaji wa uongozi wa kisiasa tuliokuwa nao na tunaoendelea kuwa nao.Katika nchi masikini kama Tanzania, uongozi wa kisiasa ni muhimu katika kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa, kukuza na kupanua demokrasia na kuhakikisha kuwa nchi inaendeshwa kwa misingi ya utawala wa sheria, ambapo haki inatendeka na inaonekana inatendeka. Utawala wa sheria na haki sawa kwa wananchi wote ndio msingi imara wa amani na utulivu. Changamoto kubwa ya nchi yetu ni kujenga uchumi unaokua kwa kasi, kuongeza ajira na kuneemesha wananchi wote.


Tanzania inakabiliwa na changamoto mbili kubwa kujenga uchumi wenye manufaa kwa wananchi wote na kujenga demokrasia ya kweli itakayohakikisha nchi inaendeshwa kwa kufuata sheria zinazotoa haki sawa kwa wananchi wote. Nchi yetu inahitaji uongozi ambao unaona siasa ni utumishi wa dhati na uliotukuka kwa umma uliozindukana na siyo nyenzo ya kukimbilia na kupigania vyeo, fursa na nguvu ya ushawishi kwa malengo ya kujilimbikizia uwezo wa maamuzi na wa utajiri binafsi usiohojiwa.

Uongozi wa nchi unawajibika kubuni sera kwa kuzingatia uhalisia na hali ya uchumi wa nchi, fursa zilizopo na vikwazo vinavyoikabili nchi katika kukuza uchumi wake.  Baada ya kubuni sera uongozi unawajibika kuzieleza sera hizo kwa wananchi na kuwahamasisha waziunge mkono na waelewe kuwa ili kujinasua toka dimbwi la umaskini wanawajibika kuchapa kazi kwa bidii, kuweka akiba, kuwa wajasiriamali wabunifu na kukubali kasi ya mabadiliko inayoendana na ukuaji wa uchumi.  Uongozi utafanikiwa ikiwa sera zake zinaaminika na zinatekelezeka, na matunda ya sera hizo yanaleta neema kwa wananchi wote.

Uongozi makini utakaoweza kuchochea maendeleo ya muda mrefu unapaswa kuwa na subira, uwe na dira na mipango ya muda mrefu na ujikite katika lengo la kukuza uchumi utakaoongeza ajira na kuleta neema kwa wananchi wote. 

Katika zama za demokrasia ya vyama vingi ni muhimu kwa wadau vikiwemo Vyama Vya Siasa kukubaliana alau kwa ujumla dira ya maendeleo ya nchi na kila chama kitakachoingia madarakani kitekeleze sera zitakazokuza uchumi unaoleta tija na neema kwa wananchi wote.  Watendaji wazuri wa serikali walio waadilifu na uwezo mzuri wanasaidia sana katika kushauri wanasiasa walioko madarakani sera zinazotekelezeka na zenye manufaa kwa wananchi.

Baada ya muda mrefu bila ya kuwa na maendeleo ya kutosha, urekebishaji wa sera ni jambo muhimu.  Hata hivyo kurekebisha siyo lengo la mwisho.  Lengo ni matunda yanayotokana na kurekebisha sera hizo.  Nchi zilizofanikiwa kupata maendeleo ya muda mrefu, zimetegemea na kuutumia mfumo wa uchumi wa soko. Kuutegemea na kuutumia Uchumi wa soko hakumaanishi kuwa soko huria pekee ndiyo chanzo cha kukua uchumi.  Serikali madhubuti zilijenga mazingira ya kuwezesha sekta binafsi kutumia uchumi wa soko kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi.

Uchumi wa soko ulioendelea unajikita katika historia na asasi muhimu katika jamii husika.  Asasi hizo ni pamoja na kuwepo haki na uhuru wa kumiliki mali, mikataba, hususan katika shughuli za biashara na uchumi huheshimiwa na inapovunjwa kuna mamlaka zinazosuluhisha na kuhakikisha kuwa mikataba inasuluhishwa kwa gharama za wastani wa wale wenye haki wanapata fidia na hawadhulumiwi.  Taarifa kuhusu masoko zinawafikia wadau wote.

Katika hatua za awali za kutafuta na kuleta maendeleo, serikali makini zinafanya majaribio ya sera zake katika maeneo machache kabla ya utekelezaji katika nchi nzima.  Moja ya mapungufu makubwa katika kubuni na kutekeleza sera katika Tanzania ni ukosefu wa kufanya majaribio na kupima mafanikio yake kabla ya kutekeleza nchi nzima.  Matatizo haya yalikuwa makubwa wakati wa sera za ujamaa.  Kwa mfano sera za kuhamia vijiji vya kudumu kuwa ni amri mwaka 1974, Sera ya elimu kwa msingi kwa wote katika mwaka mmoja, sera ya kufunga maduka binafsi na kadhalika zilitekelezwa kabla ya kufanyiwa majaribio.  Hivi karibuni sera ya kuanzisha shule za sekondari za kata haikufanyiwa majaribio kabla ya kuitekeleza nchi nzima.  Ni muhimu katika utekelezaji wa sera, serikali ikafanya majaribio (pilot projects) na kujifunza katika majaribio hayo kabla ya kuitekeleza sera katika eneo kubwa.

Kubuni sera nzuri ni mwanzo tu.  Sera zinazopaswa kuwekwa katika mipango ya utekelezaji na kutekelezwa kwa umakini wa hali ya juu.  Utekelezaji na matokeo yake yafanyiwe tathmini ya mara kwa mara ili makosa yangunduliwe na kurekebishwa.  Kujenga utumishi bora, wenye ujuzi, usiyoyumbishwa na rushwa ndani ya serikali ni changamoto muhimu.  Utumishi mzuri ulio imara haujengwi siku moja.  Viongozi wa kisiasa ni wepesi kuhujumu kuwepo kwa utendaji mzuri serikalini ikiwa watawatumia watendaji wa serikali kufanikisha malengo ya kisiasa ya kubaki madarakani kwa kuiba kura wakati wa uchaguzi au utekelezaji wa miradi ya muda mfupi kwa malengo ya kuvutia wapiga kura.  Serikali inawajibika kuvutia watumishi wenye uwezo na ari ya kufanya kazi.  Ni muhimu mishahara ya wafanyakazi serikalini iwe inavutia lakini utunishi serikalini uzingatie uwezo na siyo mtoto wa nani au unamjua nani!

Serikali yenyewe siyo inayoleta ukuaji wa uchumi.  Kazi hiyo kwa sehemu kubwa ni ya sekta binafsi yenye wajasiriamali wazuri wanaowekeza na kutumia teknolojia bora na kuzitumia fursa zilizopo katika uchumi wa soko.  Hata hivyo serikali adilifu, yenye sera nzuri zinazojulikana na kutekelezwa kwa makini, isiyoyumba ni muhimu sana kwa maendeleo ya muda mrefu.  Kazi muhimu ya serikali ni pamoja na kuhakikisha kuna utulivu katika uchumi mpana kwa maana ya kutokuwepo mfumko wa bei kuwepo kwa akiba ya kutosha na fedha za kigeni kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nchi za nje, matumizi ya serikali na sekta ya umma yalingane na mapato ya serikali, na serikali iwekeze katika miundo mbinu muhimu.

Nchi zilizofanikiwa kukuza uchumi kwa muda mrefu zinafanya hivyo kwa kuwa na sera zinazoenda na mabadiliko ya uchumi ndani na nje ya nchi.  Mikakati ya kukuza uchumi ibadilike kufuatana na mabadiliko ya mfumo wa uchumi.  Siasa za ndani ya nchi pia zinastahiki kubadilika na kwenda na wakati.  Kukua kwa uchumi kutaongeza idadi ya watu wenye kipato cha kati na watu wenye elimu ambao watadai kushiriki katika maamuzi ya sera zinazowagusa na kuwa na sauti nchi yao.

Sera za kurekebisha uchumi ili kuchochea ukuaji wake na maeneo ya kuwekeza katika miundo mbinu ni mengi na yanazidi uwezo wa mapato ya serikali. Mkakati wa kukuza uchumi lazima uweke vipaumbele vya maeneo ambayo serikali itayashughulikia mwanzo.

Sera za kukuza uchumi endelevu zinajenga, mazingira mazuri ya uwekezaji mkubwa wa vitega uchumi, ongezeko la ajira, ushindani wa kibiashara, wepesi wa raslimali kutumiwa kwa shughuli mbadala (mobility of resources) hifadhi ya jamii na wananchi wote kufaidi matunda ya kukua kwa uchumi.

Hakuna nchi iliyofanikiwa kukuza uchumi kwa kasi ya juu kwa muda mrefu bila serikali kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika miundo mbinu – barabara, nishati, reli, bandari na mawasiliano, elimu na afya.  Uwekezaji wa serikali  katika sekta ya miundo mbinu, elimu na afya unajenga msingi imara unaovutia sekta binafsi kuwekeza katika shughuli za uzalishaji na biashara.  Uwekezaji wa sekta ya umma katika maeneo hayo unatengeneza njia yakuwezesha viwanda na makampuni mapya kuanzishwa na kuongeza faida ya shughuli zote za kibiashara zinazofaidika kwa kuwepo wafanyakazi wenye afya njema na walioelimika, kuwepo kwa barabara nzuri zinazopitika wakati wote, na kuwepo kwa umeme wa uhakika.

Nchini Tanzania, uwekezaji katika miundombinu umekuwa mdogo na hutegemea fedha za misaada toka nje.  Ukarabati wa miundo mbinu haufanyiki ipasavyo.  Barabara inajengwa inatumiwa mpaka inaharibika kabisa.  Ili ikarabatiwe tunaomba msaada kwa wafadhili waijenge upya.  Mifano ni Mingi.  Barabara ya Mandera, Barabara ya Dar es Salaam - Morogoro, Barabara ya Chalinze – Segera – Tanga, n.k

Ukuaji wa uchumi unaambatana na mabadiliko ya mfumo wa uchumi kutoka kutegemea sana kilimo na kuelekea kwenye ongezeko la ajira viwandani, kutoka nguvu kazi inayoishi vijijini kuelekea nguvu kazi inayoishi mijini.  Mabadiliko ya mfumo wa uchumi husababishwa na ushindani wa soko.  Serikali zenye malengo ya kukuza uchumi endelevu zinawajibika kujenga ushindani katika masoko yote kuruhusu makampuni mapya yenye tija kuanza na makampuni yanayopata hasara kufilisika.  Soko la ajira liwe jepesi kuruhusu makampuni mapya kuajiri wafanya kazi na makampuni yanayopata hasara kupunguza wafanyakazi.  Sheria za kazi zijikite katika kurahisisha uanzishwaji wa ajira. Ni muhimu sana kuwa na utaratibu wa hifadhi za jamii kwa wafanya kazi wanaopoteza ajira ili kupunguza makali na kuwepo kwa soko la ajira linalonyumbulika.  Wanaopoteza ajira wapate kipato cha kuwawezesha kuishi wakati wakitafuta ajira mpya.

Elimu bora inayowapa wafanyakazi uwezo wa kujifunza na kupata ujuzi mpya ni kinga muhimu ya kutopoteza ajira kwa muda mrefu.  Vile vile zinaongeza kasi ya ajira mpya kuanzishwa kwa wingi na kwa hiyo kuhakikisha nguvu kazi inaajiriwa. 

Mkakati wa kukuza uchumi lazima uzingatie kuwa toafuati kubwa za vipato vya wananchi kati ya maskini na matajiri havisaidii ukuaji wa uchumi na vinaongeza upinzani dhidi ya sera za kurekebisha uchumi.  Ni wazi uchumi unapoanza kukua tofauti za vipato zinaongezeka.  Sera zijikite katika kutoa fursa ya kupata ajira kwa wananchi wengi iwezekanavyo  na misaada maalum itolewe kwa watu maskini waweze kujinasua toka dimbwi la umaskini.  Vurugu za kisasa kupinga wachache kuwa matajiri wakati wengi ni maskini zitaathiri mikakati ya kukuza uchumi.

Kigezo muhimu cha kupima kama sera zinatoa fursa sawa kwa wote ni fursa za wasichana kupata elimu iliyo bora.  Wanawake walipata elimu, wanakuwa na watoto wachache wenye afya bora ambao wanawazaa wakati maungo yao yamekua.  Kina mama wenye elimu wanasisitiza na kuhakikisha kuwa watoto wao nao wanapata elimu.  Kuwaelimisha wasichana na kuwapa fursa ya kupata ajira ni nyenzo madhubuti ya kuutokomeza umaskini.

Nchi zilizofanikiwa kukuza uchumi kwa kasi zilitumia vizuri fursa zilizopo katika soko la dunia na kuongeza uuzaji wa bidhaa zao za viwandani katika soko hilo.  Sera za kuongeza uzalishaji wa bidhaa za viwanda hazikutegemea utaratibu wa soko huria tu.  Serikali zilijaribu sera mbali mbali za kutoa motisha wa kuongeza uzalishaji viwandani na kuuza bidhaa za viwandani nchi za nje.  Sera za kukuza sekta ya viwandani ni pamoja na ruzuku katika uzalishaji wa bidhaa mpya, uwekezaji wa miundo mbinu mizuri katika maeneo maalum ya kuanzisha viwanda vipya, misamaha ya kodi.  Ni muhimu motisha maalum kwenye viwanda vitakavyouza bidhaa nchi za nje zisiwe za kudumu.  Ikiwa sera hazikufanikiwa kuongeza kasi ya kukua kwa sekta ya viwanda na uuzaji wa bidhaa nchi za nje, sera hizo zibadilishwe.

Utandawazi umefanya uchumi wa dunia hivi sasa kuwa wazi zaidi na kuingiliana sana katika biashara, uwekezaji, huduma za fedha na teknolojia.  Nchi zilizokua kwa kasi ya juu zimefanya hivyo kwa kuingiza maarifa, teknolojia na ujuzi kutoka nchi za nje.  Njia moja ya kupata maarifa na teknolojia kutoka nje ni kupitia uwekezaji unaofanywa na makampuni ya nje.  Njia nyingine ni kupata elimu, maarifa na teknolojia iliyopo katika nchi zilizoendelea na kuitumia kwa kuzingatia uhalisi na mazingira ya nchi yako.

Uchumi wa dunia unatoa fursa ya soko kubwa kwa nchi zinazoendelea. Kinadharia, Tanzania inaweza  kuuza bidhaa zote za viwandani inazozalisha kwa bei ya soko la dunia. Suala la msingi ni je kuuza nchi za nje ndiyo njia pekee ya kukuza uchumi au tunaweza kukuza uchumi kwa kutegemea soko la ndani ya nchi?

Mikakati ya kuendeleza uchumi kwa kutumia soko la ndani inaweza kufanikiwa kwa muda mfupi hasa kwa nchi kubwa zenye watu wengi.  Zaidi ya hapo matatizo ya kutetereka uchumi yanaweza kutokea ikiwa nchi itafungua mipaka yake ghafla kwa bidhaa kutoka nje.  Hata hivyo mikakati ya uchumi inayotegemea soko la ndani tu hufikia ukomo wake mapema. Soko la ndani ni dogo mno kuendeleza ukuaji wa uchumi kwa muda mrefu na hautoi fursa ya kujikita na kubobea katika eneo la uzalishaji ambalo nchi ina ushindani au inaweza kujijengea ushindani mkubwa.

Ukuaji wa haraka wa uchumi katika nchi maskini hutegemea upatikanaji wa ajira kwa nguvu kazi ya ziada iliyomo nchini. Kwa kadri uchumi unavyokua ndivyo unavyoajiri nguvukazi ya ziada iliyomo nchini hasa vijijini katika sekta ya kilimo na iliyoko mijini katika sekta isiyo rasmi yenye tija ndogo.  Raslimali za nchi hasa nguvu kazi ni lazima ziwe tayari kuhama toka eneo au sekta yenye tija ndogo kwenda kwenye eneo na sekta zenye tija kubwa ambazo kwa kawaida huanzishwa mijini ambako ni rahisi kupata watu wengi wenye ujuzi na huduma muhimu kwa viwanda kama vile umeme na maji.  Ukuaji wa uchumi huambatana na ukuaji wa miji na nguvu kazi kuhamia mijini. Hata hivyo ili miji iwe vitovu vya ukuaji endelevu ya uchumi inahitaji miundombinu mizuri.

Sera za kukuza uchumi ni lazima zizingatie kuweko na utulivu katika uchumi mpana kama vile kuepukana na mfumko wa bei, ukosefu wa fedha za kigeni, ulimbikizaji mkubwa wa madeni ya sekta ya umma unaotokana na nakisi katika bajeti ya serikali na hasara za mashirika ya umma.  Vile vile mkakati wa uchumi unapaswa kutoa motisha kwa wajasiliamali, wadogo, wa kati na wakubwa kuwekeza katika sekta mbali mbali kwa kuwahakikishia kuwa wakifanya shughuli zao kwa ufanisi na kufanikiwa kupata faida, faida yao hiyo haitaporwa na vyombo vya dola au majambazi.  Vile vile ni muhimu kuwa na mikakati ya hifadhi ya jamii ya kupunguza makali ya maisha kwa watu watakao athirika na mabadiliko ya uchumi.

Kwa nchi zenye ziada ya nguvu kazi ukomo wa kasi ya kukua kwa uchumi unategemea kasi ya uwekezeshaji wa vitega uchumi.  Uwekezaji wa vitega uchumi hutegemea ukubwa wa akiba.  Ili uchumi ukue kwa kasi nchi inapaswa iweke akiba alau asilimia 25 – 30 ya pato la Taifa na kulimbikiza vizuri katika vitega uchumi vyenye tija kubwa.  Misaada kutoka nje haiwezi kuwa mbadala wa juhudi za kuweka akiba za ndani ya nchi za kila kaya, sekta binafsi na sekta ya umma ili akiba ilimbikizwe katika vitega uchumi muhimu.

Hivi sasa nchi yetu inakabiliwa na ombwe la uongozi na tumeshindwa kutumia raslimaliwatu na maliasili yetu kujenga uchumi unaoongeza ajira na kutokomeza umaskini. Nchi inahitaji uongozi utakaowaunganisha Watanzania kukabiliana na changamoto nilizozianisha katika mada hii. Watanzania tunapaswa kujiuliza bila kujali, itikadi, udini, ukabila na umajimbo nani katika viongozi wetu wa kisiasa wana dira na uwezo wa kuwaunganisha Watanzania kutekeleza dira ya mabadiliko itakayojenga uchumi imara, unaongeza ajira na kutokomeza umaskini? Tukiipoteza fursa ya kulijibu swali hili kwa vitendo mwaka 2015, tunaweza kujikuta tunapoteza miaka mingine 50 ya uhuru wetu bila kujiletea maendeleo na wananchi wengi kiendelea kubakia maskini wa kutupwa.

KAULI YA NAPE DHIDI YA CHADEMA NI KAMA MTU ANAEOGOPA KIVULI CHAKE

Mh Abdul Kambaya-
Naibu Mkurugenzi wa Habari,
Mahusiano na Haki za Binadamu
wa Chama cha Wananchi (CUF)
CUF –Chama cha Wananchi kimeshangazwa na Kauli ya Katibu Muenezi wa CCM, alietoa kwa Vyombo vya Habari na kukituhumu chama cha CHADEMA , kwamba kimeingia mikataba ya kufisadi na Wafadhili walionje ya Nchi kwa lengo la kutaka kuja kupora Mali ya Asili inayoendelea kugunduliwa hapa Nchini kwetu Tanzania. Katika maelezo yake Katibu huyo iliita kile kilichofanywa na CHADEMA katika HARAMBEE ya kutafuta Fedha ni USANII, na kwamba CHADEMA wanataka kuhalalisha mabilioni waliopata toka kwa Wafadhili wao, na kwamba CCM inaushahidi na inawafahamu Wafadhili hao.
CUF –Chama cha Wananchi kinashangazwa na kauli hii ya kisanii iliotolewa na CCM kupitia Katibu wake Muenezi, CCM ni Chama kinachoongoza Nchi, jambo ambalo walipaswa kusema sio kuishitaki CHADEMA kwa Wananchi bali ni kuzuia hayo babilioni na kuwataja hao wafadhili ambao wameingia Mikataba na CHDEMA kwa lengo la kuja kupora utajiri mkubwa unaoendelea kugunduliwa katika masiku ya hivi karibuni. CUF- Chama cha Wananchi kinaamini kwamba CCM na CHADEMA ni watoto wa familia moja , na Wanafadhili wanao wafadhili ni wa aina moja wa ndani na nje ya Nchi. Iwapo Chadema wameingia mikataba ya kupewa mabilioni ili baadae wataposhika Madaraka waweze kulipa mabilioni hayo kwa kutukmia Mali ya asili tulionayo, basi watakuwa wanaendeleza utaratibu ule ule wa CCM wa kuiuza Nchi kwa bei poa ili mradi wao wawepo madarakani kama ambavyo CCM inafanya hivi sasa kuingia Mikatba mibovu isiokuwa na Manufa na Wananchi ili mradi wao wawafurahishe Wafadhili wao.
CUF- Chama cha Wananchi kinaamini kwamba Mti wa Matatizo ya Nchi yetu, ni Mufumo mbovu unaoendesha Serikali yetu na Nchi kwa ujumla wake. Kuwa na Vyama vyenye tamaa ya Madaraka, kama CCM na Chadema, ni matokeo ya awali ya Mfumo mbovu wa Nchi yetu, na kukithiri kwa wizi na matumizi mabaya ya Fedha za Umma na ukiukwaji wa Haki za binaadamu ni matokeo ya kati ya Mfumo mbovu. Watanzania waliowengi kuwa masikini wa kutupwa, ukosefu wa huduma bora kwa jamii,kudumaa kwa maendeleo ya Nchi na ukosefu wa ajira ni Matokeo ya muda mrefu yanayosababishwa na Mfumo mbovu wa Nchi yetu. Kwa maana hiyo basi, CUF –Chama cha Wananchi kinaamini kwamba , njia sahihi ya kulinda Rasilimali zilizopo na zinazoendelea kugunduliwa ndani ya Nchi yetu, ni kuwa na Serikali ya Umoja wa Kitafa, Serikali ambayo itashirikisha Vyama vyote venye wabunge, na kwa utaratibu huo, kutakuwa hakuna Chama kitakachokuwa na maauzi ya pekee katika matumizi ya Rasilimali na Mali ya asili ya Nchi yetu. Jambo hili limekuwa linahubiriwa sana na CUF , lakini pia limekuwa linapingwa sana na CCM na Chadema na kwa mantiki hiyo,
CUF – Chama cha Wananchi hakioni tafauti ya CCM na Chadema kisera na kimtazamo. CUF kinawataka Watanzania waelewe kwamba, kinachonekana hapa ni kwamba ,Chadema inaonyesha imewazidi kete CCM huko kwa Wafadhili wa nje kama ilivyowazidi kete kwa ufadhili wa Sabodo ndio maana unaona CCM inapiga kelele.
CUF – Chama cha Wananchi kina wataka CCM waache kuogopa kivuli chao na badala yake washughulike na kubadili Mufumo unaoendesha Nchi yetu iwapo kweli wanataka mabadiliko ya Kiuchumi na Kijamii .

Thursday, August 16, 2012

Kuporomoka kwa uchumi wa dunia na mikakati ya Tanzania kujikwamua kiuchumi


Mwenyekiti Wa Cuf Taifa-Prof Ibrahim Haruna Lipumba

Uchumi wa nchi muhimu zilizoendelea ikiwemo Marekani, Jumuia ya Ulaya na Japan bado unayumba miaka minne baada ya mtikisiko mkubwa wa uchumi mwaka 2008. Mtikisiko huo ulisababishwa na sera mbovu ya usimamizi wa sekta ya fedha ilioruhusu mfumko wa bei za nyumba na uwekezaji mkubwa katika sekta hiyo. Tufe la mfumko wa bei za nyumba lilipopasuka na bei hizo kuporomoka, mabenki mengi yalikabiliwa na tatizo la kufilisika kwa sababu mikopo yao katika sekta ya nyumba haikuweza kulipika na amana zilizohusiana na sekta ya nyumba ziliporomoka. Familia nyingi zilikopa kwa kutumia thamani ya nyumba zao kama dhamana. Kuporomoka kwa bei za nyumba ziliondoa uwezo wa kukopa na kuwalazimisha walipe madeni yao na kwa hiyo kupunguza matumizi ya kununua bidhaa na huduma. Familia zinapopunguza matumizi ya kawaida makampuni yanayotengeneza bidhaa na kutoa huduma yanakosa soko na kulazimika kupunguza uzalishaji wa bidhaa na huduma na kupunguza wafanyakazi. Watu wa kikosa ajira wanapunguza matumizi na hivyo kuathiri uzalishaji wa bidhaa na huduma na kuchochea uachishwaji wa kazi wa watu wengi zaidi. Makampuni yanayoshindwa kuuza bidhaa zao yanapunguza wafanyakazi na yanaacha kuwekeza vitega uchumi kupanua shughuli zao kwa ukosefu wa soko la bidhaa na huduma zao. Kupunguza uwekezaji kunaongeza ukosefu wa ajira.
Mahitaji ya soko la bidhaa na huduma yanapopungua, Benki Kuu inaweza kusaidia kuongeza mahitaji hayo kwa kupunguza riba. Riba inapopungua gharama za mikopo inakuwa rahisi na kwa hiyo familia na wawekezaji wanaweza kukopa. Katika mtikisiko wa uchumi ulioanza mwaka 2008, riba za Benki Kuu zimepunguzwa mpaka kufikia karibu ya sufuri na kwa hiyo haziwezi kupunguzwa zaidi ya hapo. Uwezo wa sera za riba kusaidia kuongeza matumizi ya sekta binafsi na kaya umetoweka kwa sababu riba za Benki Kuu haziwezi kwenda chini ya sufuri. Zaidi ya hapo ikiwa makampuni hayana imani kuwa kutakuwa na ongezeko la mahitaji ya bidhaa zao, hawewezi kuongeza uwekezaji hata kama riba ni za chini.
Benki Kuu inaweza kuongeza matumizi ya kaya na sekta binafsi ikiwa itaonyesha kuwa sera zake zitaongeza mfumko wa bei. Ikiwa mfumko wa bei ni wa juu, akiba ya fedha taslimu inapungua thamani yake. Watu watabaini kuwa vyema kununua bidhaa za kudumu kuliko kuweka akiba ya pesa taslimu. Wachumi wengi wamependekeza sera hii ya kuongeza mfumko wa bei kutoka asilimia 2 na kufikia asilimia 4. Hata hivyo Benki Kuu nyingi za nchi zilizoendelea zinaongozwa na mahifidhina wanaoamini kuwa jukumu lao kubwa ni kuhakikisha mfumko wa bei hauzidi asilimia 2. Hawaikubali kabisa sera itakayoongeza mfumko wa bei kwa muda ili kuhamasisha sekta binafsi inunue bidhaa na huduma badala ya kuweka akiba.
Katika hali ya ukosefu wa soko la kuuza bidhaa na huduma kila kampuni inafanya uamuzi wa busara wa kupunguza matumizi na uwekezaji. Familia zinazokabiliwa na kupungua kwa utajiri walionao na kuongezeka kwa madeni wanaamua kupunguza matumizi na kuongeza akiba. Uamuzi wa familia moja moja na kampuni moja moja una mantiki lakini kwa pamoja kila familia na kampuni zikipunguza matumizi pato lao la pamoja linapungua kwani matumizi yako ndiyo mapato ya mwingine. Ili kukabiliana na tatizo hili serikali ya nchi zilizoendelea zinawajibu wa kuongeza matumizi kuziba pengo lililoachwa na sekta binafsi. Serikali inaweza kuongeza matumizi kwa kuongeza nakisi ya bajeti. Sekta binafsi inapokuwa na kipato kidogo, mapato ya serikali ambayo yanatokana na kodi yanapungua. Kuongeza matumizi wakati mapato yanapungua maana yake ni kuongeza nakisi ya bajeti na kwa hiyo kuongeza deni la serikali. Sera ya kuongeza matumizi ya serikali na nakisi ya bajeti ni ya muda mfupi.Uchumi ukiimarika serikali itakusanya kodi nyingi na pia ina fursa ya kupunguza matumizi na kwa hiyo kuwa na ziada katika bajeti yake na kupunguza deni lake.
Sera za kuongeza matumizi ya serikali na hivyo kuwa na nakisi ya bajeti kubwa na kuongeza deni la serikali imepingwa na wahafidhina. Nchini Marekani Chama cha Republican ambacho kina Wawakilishi wengi katika Baraza la Wawakilishi kinapinga kuongeza matumizi ya serikali kwa madai kuwa itaongeza nakisi na kuongeza deni la taifa. Sera za nchi za Jumuiya za Ulaya, kanda ya euro zinaongozwa na fikra za Serikali ya Ujerumani ambayo inapinga serikali kuwa na nakisi kubwa ya bajeti. Nchi wanachama wa kanda ya euro hawana Benki Kuu zao zilizo huru na hawana sarafu zao wenyewe. Hawana uwezo wa kuongeza nakisi ya bajeti zao bila kuongeza riba. Serikali za nchi za Ulaya Kusini – Hispania, Italia, Ureno na Ireland wanalipa riba kubwa sana wanapokopa katika masoko ya fedha. Uingereza ambayo nakisi yake ya bajeti ni kubwa zaidi ya Hispania inatozwa riba ndogo kwa sababu ina Benki Kuu na  sarafu yake yenyewe na kwa hiyo ina uwezo wa kulipa madeni yake kwa kuchapisha fedha zake kwa wingi.
Hatua za mwanzo za kukabiliana na mtikisiko wa uchumi mwaka 2008 ulikuwa sahihi. Nchi nyingi ziliongeza matumizi ya serikali. Kwa sababu ya itikadi za kihafidhina, kuongezeka kwa nakisi ya bajeti na kukua kwa deni la taifa likaleta mabadiliko ya sera serikali zikaanza kubana matumizi kabla ya uchumi kutengamaa na sekta binafsi kuimarika. Sera sahihi ni kuendelea kuongeza matumizi ya serikali katika kipindi cha muda mfupi na kuweka mpango wa kukabiliana na nakisi ya bajeti na deni la serikali kwa muda wa kati baada ya sekta binafsi kuimarika na hivyo kuongeza ajira na kodi za serikali. Misamaha ya kodi kwa matajiri iondolewe wakati wananchi wenye kipato cha chini na cha kati waendelee kunufaika na misamaha ya kodi katika kipindi cha muda mfupi mpaka uchumi utakapoimarika.
Baada ya mgogoro wa fedha duniani wa mwaka 2008, jumla la pato la dunia lilianguka kwa asilimia 0.6 mwaka 2009. Uchumi wa nchi zilizoendelea ndiyo ulioanguka zaidi. Pato la taifa la Ujerumani lilianguka kwa asilimia 5.1, Japan na Italia kwa asilimia 5.5, Uingereza asilimia 4.4 na Marekani kwa asilimia 3.5. China haikuathirika sana na mtikisiko wa uchumi wa dunia kwa sababu ya hatua zilizochukuliwa na serikali ya China za kuongeza matumizi kukabiliana na kupungua kwa mahitaji katika soko la bidhaa. Kasi ya kukua kwa pato la taifa la China ulipungua kutoka asilimia 14.2 mwaka 2007 na kufikia asilimia 9.2. Juhudi za pamoja za  kufufua uchumi za Marekani, nchi za Jumuiya ya Ulaya na nchi zinazoendelea hasa Uchina, India na Brazil zilisaidia kuongeza ukuaji wa uchumi wa dunia na kufikia asilimia 5.3 mwaka 2010. Lakini kupunguza kwa matumizi ya serikali na mgogoro wa Euro umepunguza ukuaji wa uchumi na kufikia asilimia 3.9 mwaka 2011 na makadirio ya 3.5 mwaka 2012.
Nchi za Jumuiya ya Ulaya zinakabiliwa na mdororo mwingine wa uchumi kwa sababu ya matatizo ya Euro. Pato la kanda ya Euro linakadiriwa kupungua kwa asilimia 0.3 mwaka 2012. Nchi za Ulaya ya Kusini – Ugiriki, Hispania, Italia na Ureno ndizo zimeathirika zaidi kwa kuporomoka kwa uchumi na kuongezeka kwa ukosefu wa ajira. Pato la taifa la Marekani litakua kidogo tu kwa asilimia 2.1. Ukosefu wa ajira unabakia juu sana zaidi ya asilimia 8.0.
Inasikitisha kuwa nchi zilizoendelea zimekumbwa na itikadi ya kihafidhina na wameshindwa kufuata ushauri wa wachumi wa kimataifa wa kuongeza matumizi ya serikali katika kipindi cha muda mfupi na kushughulikia nakisi ya bajeti na ukuaji wa deni la taifa katika kipindi cha muda wa kati. Kususua kwa uchumi wa nchi zilizoendelea kunaongeza matatizo kwa nchi maskini katika mikakati yao ya kukuza uchumi, kuongeza ajira na kuutokomeza umaskini. Nchi maskini kama Tanzania inategemea soko la nchi zilizoendelea kuuza bidhaa zake, wengi wa watalii wanaokuja Tanzania wanatoka nchi za Ulaya, Wawekezaji wa vitega uchumi wanatoka nchi zilizoendelea na serikali inategemea misaada na mikopo toka nchi hizo.
Kati karne ya 21 nguvu za uchumi za mataifa umeanza kubadilika. Uwezo wa kiuchumi wa nchi za magharibi unapungua ukilinganisha na nchi za Asia. Nchi nyingi zinazoendelea na hasa China zimeendelea kukuza uchumi wao pamoja na kuathiriwa na mtikisiko wa uchumi wa nchi zilizoendelea. Nchi yetu inabidi iweke mkakati wa kushirikiana na nchi zinazoibuka na kuwa na nguvu za kiuchumi kwa manufaa ya nchi yetu lakini tusigezwe kuwa soko la bidhaa duni toka nchi hizo.
Kwa kuwa nchi yetu iko nyuma katika maendeleo ya uchumi, tuna fursa nyingi za kutumia elimu, utaalamu na teknolojia ambayo imeishagunduliwa ili tukuze pato letu la taifa, tuongeza ajira yenye kipato kizuri, na hatua kwa hatua tuotokomeza umaskini. Ni muhimu kwa Watanzania tujihamasishe na tuwe na motisha wa kujifunza na kutumia teknolojia iliyopo tukizingatia mazingira tuliyonayo. Kuna fursa kubwa ya kuongeza uzalishaji na tija kwa kutumia teknolojia bora katika sekta ya kilimo, mifugo, uvuvi, misitu, madini, nishati, viwanda, usafiri na mawasiliano, na huduma za jamii.
Kuwepo kwa fursa za kukuza uchumi katika sekta mbalimbali hakuna maana kuwa fursa hizo zinaweza kutumiwa kirahisi. Kuwa na uchumi wa soko na utengamano wa uchumi mpana (macroeconomic stability), fedha za kigeni kupatikana kwa bei ya soko na kuondoa vikwazo vya biashara ya nje hakutoshi kuiwezesha nchi kukua kwa asilimia 8-10 kwa muda wa miaka 20-30 na kuubadilisha mfumo wa uchumi wake kutoka kutegemea kilimo na sekta isiyo rasmi na kuongeza ajira katika sekta ya viwanda na huduma za kisasa.  Kukua kwa uchumi kwa kasi hiyo kunahitajika ili kuhakikisha tunautokomeza umaskini.
Tunahitaji sera za maksudi za kuasisi maendeleo makubwa ya viwanda kwa kuanzia na viwanda vinavyotumia malighafi inayozalishwa nchini. Kuanzisha na kuendeleza viwanda hakutafanikiwa kwa kuachia mfumo wa soko peke yake uamue maeneo ya uwekezaji. Juhudi maalum ya serikali na nidhamu ya hali ya juu ya utekelezaji inahitajika. Serikali inapaswa kutambua vikwazo vinavyokwamisha maendeleo ya viwanda na kuviondoa. Miundombinu ya usafiri na umeme ni muhimu kwa maendeleo ya kasi ya viwanda na uchumi kwa ujumla. Pamoja na kuelewa kuwepo kwa tatizo hili kwa muda mrefu, inasikitisha kuwa serikali imeshindwa kabisa kutekekeleza mipango yakutatua matatizo ya miundombinu. Serikali imeshindwa kuweka vipaumbele na kutekeleza miradi michache ikakamilika kabla ya kuanza miradi mingine.
Serikali imekuwa na mipango mingi isiyo tekelezwa au kutekelezeka. Kuna Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025 ambayo inalenga kuwa Tanzania iwe ni nchi yenye kiwango cha kati cha mapato (middle income country) na hali bora ya maisha kwa wananchi. Mpango Maalum wa Kuharakisha Maendeleo ya Tanzania (Tanzania Mini Tiger Plan 2020) ambao haijulikani umeishia wapi.  Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania – MKUKUTA I na MKUKUTA II na Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano 2010-15. MKUKUTA I na MKUKUTA II hazikufanyiwa makadirio ya gharama za utekelezaji wake. Gharama za mpango wa miaka mitano ni kubwa mno na serikali haina fedha ya kuugharamia.
Pamoja na matatizo ya uchumi wa dunia, Tanzania inaweza ikatumia fursa ya kuwa nyuma na kutumia teknolojia iliyopo kukuza uchumi wake. Watanzania tunahitaji tutafakari hali halisi tuliyonayo na tubuni sera na mikakati ya pamoja inayotekelezeka ili tujikwamue toka dimbwi la umaskini. Misingi muhimu ya sera na mikakati hiyo iwe kuitumia vizuri mali ya asili ya Tanzania kwa manufaa ya wananchi wote huku tukilinda mazingira yetu. Kuwekeza kwenye afya ya watoto wa Tanzania toka wakiwa katika mimba za mama zao kwa kuhakikisha kina mama wajawazito na watoto wachanga wanapata lishe bora. Kuwekeza katika elimu ya watoto wa Tanzania toka shule za chekechea na kuendelea. Kuweka msisitizo maalum katika elimu ya hesabu, sayansi na teknolojia. Kuwekeza katika kilimo hasa cha chakula kama vile mahindi, mpunga, maharage, jamii ya kunde na mbegu za mafuta kukidhi mahitaji ya ndani na kuuza masoko ya nje hasa nchi za jirani. Kuwekeza katika miundombinu ya barabara, umeme, maji na mawasiliano. Kuweka mkakati madhubuti wa kuanzisha na kuendeleza viwanda vinavyotumia malighafi ya ndani na kuajiri watu wengi kama vile viwanda vya nguo na mavazi, viatu na bidhaa za ngozi, vifaa vya matumizi ya nyumbani na vifaa vya umeme na elektroniki.
Kubuni na kutekeleza mikakati hii Tanzania inahitaji uongozi wenye dira utakaowaunganisha na kuwahamasisha Watanzania tujielimishe na tutumie raslimali na mali ya asili ya nchi yetu kuwaletea neema wananchi wote.

Wednesday, August 8, 2012

JUMUIYA YA VIJANA YA CUF YALAANI MAUAJI YA WANASIASA VIJANA KUKITHIRI NCHINI:

Naibu Katibu JUVICUF
Jumuiya ya Vijana ya CUF inasikitishwa na kusononeshwa na vitendo vya mauaji ya wanasiasa vijana inayoendelea hapa nchini Tanzania. Hii ni kutokana na mauaji ya kila mara ya vijana hasa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambayo yanaonekana kama mauaji ya kulipizana kisasi. Huu si ustaarabu wa kidemokrsia bali ni ukiukwaji wa haki za binadamu.
Ni hivi karibuni watanzania walishuhudia mauaji ya kikatiri ya kiongozi wa vijana wa CHADEMA kule Arusha mara baada ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki. Lakini pia tumeshitushwa na mauaji mengine ya kijana kiongozi wa CCM jimboni Iramba Magharibi juzi baada ya mkutano wa hadhara wa CHADEMA.
Mauaji ya namna hii huleta hofu kwa vijana kushiriki siasa za moja kwa moja kwa kuogopa kuuawa. Iwapo mauaji haya ya vijana wanasiasa hayatapatiwa ufumbuzi kuna hatari ya vijana wenye uwezo kuikimbia siasa na hatimaye Taifa likakosa viongozi bora wa sasa na baadaye.
Jumuiya ya Vijana ya CUF inaamini kuwa bila kuwa na utamaduni wa kuvumiliana  japokuwa tunatofautiana kimtazamo, itkikadi, dini na kabila zetu , kamwe hatutaifikia demokrasia ya kweli. Uvumilivu ni msingi mkuu wa Demokrasia ha hivyo ni wajibu wetu vijana kuacha kutumikia hisia na mihemko ya miili yetu na vyama vyetu na kuutanguliza Utanzania wetu na udugu wetu mbele.
Jumuiya ya Vijana ya CUF inawaomba vijana wa CCM na CHADEMA kuwa makini wakati tukiwa katika mchakato huu wa kuitafuta Demokrasia ya kweli inayojali misingi ya Haki za binadamu, utawala bora na ushindani wa hoja bila kuchukiana na kujenga uadui baina yetu kwani sote tuna nia ya kuijenga Tanzania yenye neema ambayo rasilimali zake zitawafaidisha watanzania wote.
Jumuiya ya Vijana ya CUF imesikitishwa sana na mauaji hayo ya vijana yanayofanywa na vijana wenyewe kwa wenyewe. Hii ni ishara kuwa Vijana wa CCM na CHADEMA hawajaiva kisiasa kwani wanashindwa kutofautisha Upinzani na Uadui. Na kutokana na mauaji haya ni wajibu wa watanzania kutambua kuwa CCM na CHADEMA hawana dira na sera za kuwafikisha watanzania kwenye neema bali wana nia ya kuwamaliza kwa kuwaua kikatiri.
Jumuiya ya Vijana ya CUF inawaomba watanzania wawe macho na mienendo ya vijana wa CHADEMA na CCM maana mauaji wanayoendelea kulipizana hayatakwisha leo wala kesho. Kwa hiyo wanapaswa kukigeukia chama chao kipenzi cha Wananchi –CUF ambacho ni chama cha makabwela na  wanyonge wa Tanzania.
Imetolewa na:
Thomas D.C Malima
Naibu Katibu Mkuu
 Sekretarieti ya Vijana-Taifa
CUF-Chama Cha Wananchi.

JUVICUF YATOA POLE KWA WANAFUNZI NA WAZAZI WA SHULE YA SEKONDARI YA MOROGORO

Naibu Katibu Wa JUVICUF
JUMUIYA ya Vijana  wa Chama Cha Wananchi-CUF (JUVICUF) inapenda kutoa pole kwa wanafunzi , wazazi na walimu wa Shule ya Sekondari ya Morogoro (Wasichana) kutokana na ajali ya moto iliyowakumba kwa baadhi ya majengo yake yakiwemo mabweni ya wanafunzi kuungua na kuteketetea kwa moto uliotokana na hitilafu ya umeme na kusabaisha zaidi ya wanafuzi 600 kuathirika kwa namna moja au nyingine.
JUVICUF inatambua kuwa japokuwa hakuna aliyepoteza maisha lakini wanafunzi wamepoteza masomo, mali, na wamekubwa na athari za kisaikolojia wakati wote wa ajali na baada ya ajali. Tunatambua nafasi yenu kama vijana wa Tanzania katika ujenzi wa Taifa lenu na mmepata ajali hii mkiitafuta elimu ili muijenge nchi yenu vizuri. Ni kutokana na umuhimu huo, ndio maana JUVICUF inaungana nanyi katika kipindi hiki cha matatizo.

JUVICUF inakubaliana na taarifa za awali za Jeshi la Polisi, wanafunzi na walimu wa shule hiyo kuwa  ajali hiyo ilitokana na miundombinu mibovu ya umeme shuleni hapo. Na kwa kuwa tatizo hili haliko katika shule ya Sekondari ya Morogoro(wasichana) pekee bali ni kwa zaidi ya shule 50 kongwe hapa nchini. Hii ni kwa sababu ya serikali kushindwa kuzipangia bajeti ya kutosha ya ukarabati kila mwaka. Shule hizi zilijengwa kabla na mara tu baada ya uhuru lakini hazifanyiwi ukarabati kabisa.

JUVICUF inaitaka serikali ifanye utafiti wa kina kwa shule zote za zamani kutokana na uchakavu mkubwa  wa miundombinu ya umeme na maji katika mazingira yake. Shule nyingi ziko taabani kwani majengo yake yamezeeka, miundombinu ya maji safi na majitaka pamoja na miundombinu ya umeme vimezeeka na kuharibika kabisa kiasi cha kuhatarisha afya na uhai wa wanafunzi na walimu wao.

Pia JUVICUF inaitaka serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais (Maafa) iangalie namna ya kuwawezesha wanafunzi hao waliopoteza nguo na vifaa vyao vya kusomea wapate nguo na vifaa vya kusomea ili waendelee kusoma bila matatizo wakati huu wa matatizo bila kuathiri ratiba za masomo yao ya kila siku.

Na ni wajibu wa serikali kuwahudumia  kimatibabu wanafunzi wote waliopatwa na majeraha pamoja mshituko wakati wa ajali hiyo ya moto shuleni hapo bila kuhitaji malipo kutoka kwa wazi/walezi wa wanafunzi hao. Hili ni jukumu la serikali siyo hisani kwao. Kwa hiyo tunaitaka serikali igharimie matibabu yao.

Leo tukio hili limetokea Morogoro Sekondari (Wasichana), kesho tukio kama hili linaweza likatokea shule nyingine na kuleta maafa makubwa. Kwa hiyo lazima serikali iwe makini kuzuia majanga kabla ya

kusubiri kuokoa pindi majanga yanapotokea. Lazima tuwe makini kulinda maisha ya vijana wetu hata kwa gharama kubwa maana ndio tegemeo letu kwa maendeleo ya Taifa letu. Ni heri kulinda maisha na ustawi wa watu wako kwa gharama kubwa kuliko kusubiri kuwaokoa kwa gharama kubwa.

JUVICUF inatambua athari kubwa zinazoweza kujitokeza endapo serikali haitakuwa makini na uboreshaji wa miundombinu ya shule zakekwani zinawakutanisha wanafunzi wengi katika mazingira mabovu yanayoweza kusababisha magonjwa ya milipuko, hitilafu za umeme au janga la aina yoyote ile.

JUVICUF inawapa pole na kuungana na wanafunzi hao pamoja na wazazi wao kwa kuwaomba wawe wavumilivu katika kipindi hiki cha matatizo.
Imetolewa na:
Thomas D.C Malima
Naibu Katibu –TAIFA
JUMUIYA YA VIJANA YA CUF (JUVICUF)






Tuesday, August 7, 2012

DIRA YA MABADILIKO – VISION FOR CHANGE: MANIFESTO YA CUF YA 2010


A Vision for Change
“Watanzania wameweka matumaini yao kwa Chama cha CUF na misingi yake ya sera ya kuleta “Haki sawa kwa wananchi wote” na “Kujenga uchumi imara unaoongeza ajira na utakaoleta neema na tija kwa wote.” Chama chetu kimekuwa ni Chama kikuu cha upinzani nchini kwa muda mrefu sasa na wananchi wanaendelea kuteseka kwa kuona matatizo yao yakizidi kuongezeka bila kuchukuliwa kwa hatua za msingi kushughulikia matatizo yao. Hali hii inawafanya wananchi wengi hasa vijana na wanawake kuwa katika shauku kubwa ya kuona utawala wa nchi yetu unabadilishwa kwa amani kupitia karatasi za kura. CUF kwa kutambua nafasi yake katika kuyaongoza Mabadiliko yanayohitajika, kikiwa siyo tu chama kikuu cha upinzani hapa nchini bali pia kutokana na mjengeko wake wa kuwa kweli ni chama cha kitaifa chenye kukubalika na chenye mtandao mpana katika pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano, imezindua DIRA YA MABADILIKO – VISION FOR CHANGE. Dira ya Mabadiliko ndiyo msingi wa ILANI yetu ya uchaguzi. Vision for Change chini ya Serikali ya CUF itatujengea Tanzania Mpya inayojali haki sawa kwa wananchi wote na itakayojenga uchumi imara unaoongeza ajira na utakaoleta neema na tija kwa wote.” Kwa kuisoma Manifesto yetu ya Uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa mwaka 2010, unaweza kupakuwa kwenye kiungo hapo chini.
 CUF Manifesto 2010