Thursday, August 23, 2012

KUPANDA KWA BEI YA CHAKULA KATIKA SOKO LA DUNIA KUWE CHACHU YA KUASISI MAPINDUZI YA KILIMO TANZANIA


Prof Ibrahim Haruna Lupumba-Mwenyekiti Wa Cuf Taifa.
Mwanzono mwa mwezi wa Agosti nilienda Tabora kumtazama na kumpa pole shangazi yangu anayeumwa. Hali ya bei ya chakula hasa mahindi ilinitisha. Kwa kawaida mwezi wa Agosti ni baada ya mavuno. Bei ya mahindi huwa bado iko chini. Debe la mahindi huwa halizidi shilingi 5000/- Mwaka huu agosti mwanzoni bei ya debe la mahindi ni shilingi 10000/-. Ifikapa Disemba bei ya mahindi inaweza kuruka na kufikia shilingi 15000/- au zaidi.
Tathmini ya serikali kama ilivyoelezwa na Waziri wa Kilimo na Ushirika katika hotuba yake ya bajeti kuwa “ Matokeo ya tathmini ya awali ya hali ya uzalishaji wa mazao ya chakula na utabiri wa hali ya chakula kwa mwaka 2012/2013 yanaonesha kwamba uzalishaji wa mazao ya chakula utafikia tani 13,572,804 ikilinganishwa na mahitaji ya chakula yanayokadiriwa kuwa tani 11,990,115 kwa mwaka 2012/2013. Taifa linatarajia kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 113 na hivyo kuwa na ziada ya tani 1,582,690. Tathmini hiyo ilibaini kuwepo na ziada ya chakula katika mikoa nane (8) ya Iringa, Rukwa, Mbeya, Kagera, Mtwara, Kigoma, Ruvuma na Morogoro; utoshelevu katika mikoa saba (7) ya Pwani, Mara, Tanga, Lindi, Mwanza, Singida na Dodoma; na uhaba katika mikoa sita (6) ya Shinyanga, Tabora, Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Dar es Salaam”
 Hali ya bei ya vyakula katika maeneo mengi ya nchi haionyeshi kuwepo kwa ziada kubwa. Vile vile hali ya biashara ya mazao ya vyakula ndani ya mipaka ya Tanzania ina vikwazo. Maeneo yenye ziada hayauzi chakula cha kutosha kwenye maeneo yenye upungufu. Bei ya mahindi  Tabora ingekuwa ya chini kama wafanyabiashara wangenunua mahindi toka Mpanda mkoa wa Rukwa na kuyauza Tabora.
Hata katika miaka ambayo chakula kilichozalishwa nchini kinaonekana kukidhi mahitaji ya taifa, ukosefu wa lishe bora ni tatizo la muda mrefu. Miaka 50 baada ya uhuru, theluthi moja  ya Watanzania ikimaanisha Mtanzania mmoja katika kila Watanzania watatu hawana lishe bora. Asilimia 44 ya watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wana utapiamlo, ni wafupi kuliko wanavyostaili kuwa kwa sababu ya kukosa chakula cha kutosha na lishe bora. Watoto wasiokuwa na lishe bora wanashindwa kujenga kinga ya mwili, maungo yao siyo imara na hawajengi ubongo wao vizuri na kwa hiyo wanakuwa wagumu  kujifunza na kufundishwa. Kuhakikisha kuwa kina mama wajawazito na watoto wote wanapata lishe bora ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele na familia, jamii na serikali kwa ujumla.
Hali ya bei ya mazao ya nafaka  hasa mahindi katika soko la dunia  inatisha. Tathmini ya Waziri wa Kilimo katika hotuba yake ya bajeti imepitwa na wakati kwani alieleza kuwa  taarifa ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (Food and Agriculture Organisation - FAO) iliyotolewa mwezi Juni 2012, inaonesha kuwa katika mwaka 2011/2012, uzalishaji wa nafaka duniani unatazamiwa kuongezeka kwa asilimia 3.2. Jumla ya tani  bilioni 2.42 za nafaka zitazalishwa ikilinganishwa na matumizi ya nafaka ya tani bilioni 2.38 kwa mwaka 2012/2013, matumizi ya nafaka kwa ajili ya chakula cha mifugo yataongezeka kwa asilimia 3.8 wakati matumizi ya chakula yanatazamiwa kuongezeka kwa asilimia moja (1). Akiba ya nafaka duniani inatazamiwa kuongezeka kwa tani milioni 36 na kufikia tani milioni 548 sawa na ongezeko la asilimia saba (7) kutoka kiwango cha mwaka jana.”
Marekani ya Magharibi ya Kati ndiyo eneo linalozalisha mahindi kwa wingi. Mwezi wa julai mwaka huu ulikuwa na joto kali katika eneo hili kuliko miaka yote 117 iliyopita tangu kumbukumbu za hali ya joto kuanza kutunzwa. Marekani kwa ujumla imekumbwa na ukame mbaya kupita yote kwa muda wa miaka 50. Marekani ndiyo inayoongoza katika kuzalisha na kuuza nafaka katika soko la dunia. Kwa sababu ya ukame uzalishaji wa mahindi na maharage ya soya utapungua sana mwaka huu na tayari bei za mahindi na soya zimevunja rekodi ya bei ya mwaka 2008.
Nchini Marekani na Ulaya mahindi yanatumika sana kama chakula cha mifugo. Mexico, nchi za Marekani ya kati na Afrika, mahindi ni chakula muhimu cha binadamu. Nchini Marekani ng’ombe analishwa kilo 30 za mahindi ili kupata kilo moja ya nyama.
Wamarekani pia wanatumia mahindi kutengeneza ethanol inayotumiwa kama petroli mbadala. Katika kila majunia 100 ya mahindi yanayozalishwa Marekani, 40 yanatumiwa kutengeneza ethanol. Mahindi yanayotumiwa kutengeneza ethanol kujaza tenki la gari ya familia ya Marekani yanatosha ugali wa mwaka mzima wa mkulima wa Tabora. Utumiaji wa mahindi kutengeneza ethanol kunaongeza bei ya mahindi katika soko la dunia.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa – FAO, Jose Graziano da Silva ameiomba Marekani kusitisha mara moja utumiaji wa mahindi kutengeneza ethanol ili kupunguza mfumko wa bei ya mahindi katika soko la dunia. Katika mwaka wa uchaguzi mkuu, Serikali ya Marekani haielekei kukubali wito wa Jumiya ya Kimataifa ya kusitisha matumizi ya mahindi kutengeneza ethanol kwa sababu wakulima wa mahindi wa Marekani ya magharibi ya kati wanaipenda sera ya kutumia mahindi kutengeneza ethanol kwa kuwa inaongeza bei ya mahindi. Majimbo yenye wakulima wa mahindi kama vile Iowa ni muhimu katika mkakati wa Rais Obama na chama cha Democrats kushinda uchaguzi Novemba 2012.
Kupanda kwa bei ya chakula duniani ni changamoto na fursa. Bei  ya chakula katika soko la dunia itaendelea kuwa juu kwa muda mrefu kwa sababu ya mahitaji ya nafaka kulisha mifugo na matumizi ya mazao kutengeneza petroli mbadala.
Kilimo chetu kimeendelea kuwa duni kwa sababu zisizokuwa na msingi. Tuna ardhi ya kutosha, mito na maziwa makubwa. Jiografia ya Tanzania inafanya nchi yetu iwe na majimbo yenye hali ya hewa tofauti. Mazao mbali mbali ya chakula na biashara yanastawi katika ardhi ya Tanzania, nchi yetu ina uwezo mkubwa wa kuzalisha mazao ya chakula na biashara kukidhi mahitaji ya ndani na kuuza nchi za nje. Lakini miaka 50 baada ya Uhuru, Tanzania haijitoshelezi kwa chakula kwa sababu ya sera na uongozi usiokuwa na dira sahihi ya maendeleo.
 Nchi yetu ina ardhi kubwa inayokubali aina mbambali ya mazao. Tunatumiai robo tu ya ardhi yote inayofaa kwa kilimo. Ardhi inayolimwa haipandwi mbegu bora. Kati ya wakulima 100 wa Tanzania, 90 wanatumia mbegu za kienyeji zisizokuwa na uwezo wa uzalishaji mkubwa. Wakulima wengi hawatumii mbolea. Mfumo wa usambazaji wa mbegu bora, mbolea na pembejeo nyingine ni hafifu sana. Utaratibu wa mikopo kwa wakulima wakununulia zana na pembejeo haupo. Chini ya asilimia 1 ya ardhi inayofaa kilimo cha umwagiliaji imeendelezwa na kutumiwa. Maeneo yenye mfumo wa umwagiliaji  hayatunzwi na kukarabatiwa na kwa hiyo hayazalishi kwa uwezo wake. Matumizi ya matrekta katika kilimo bado ni madogo sana. Kwa mfano mkoa wa Kigoma wenye ardhi kubwa, mabonde yenye rutuba mito na vijito vingi ina matrekta makubwa 25 na matrekta ya mkono 176 tu.
Tanzania imekosa sera sahihi ya kukuza kilimo na kuinua hali za maisha ya wakulima. Zana za kilimo na pembejeo haziwafikii wakulima na hata zinapowafikia huwa zimechelewa na kufika nje ya wakati. Pamoja na serikali kudai kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wetu, kilimo hakipewi kipaumbele. Tangu tupate uhuru wa taifa letu matumizi halisi ya sekta ya kilimo ya kila mwaka hayajawahi kuzidi asilimia tano ya bajeti yote ya Serikali. Nchi yetu haina huduma bora kwa ajili ya kukuza kilimo cha kisasa na kwa ujumla kumekuwa na udhaifu mkubwa hasa katika maeneo ya uwekezaji kwenye tafiti, motisha kwa wakulima ili wajaribu mambo mapya, ushauri na utaalamu kwa wakulima, mikopo ya zana za kilimo na pembejeo, barabara na mawasiliano vijijini.
Hatua za muda mfupi za kukabiliana na ongezeko kubwa la bei katika baadhi ya wilaya za Tanzania ni kuruhusu na kurahisisha biashara ya ndani ya mazao ya chakula. Serikali irahisishe mfumo wa kodi na ushuru wa mazao ya kilimo; ikiwa ni pamoja na kufuta ushuru na ada zote za mazao katika ngazi ya mkulima ili kuongeza motisha kwa wananchi kuwekeza juhudi zaidi katika uzalishaji wa mazao ya kilimo. Vizuizi vyote visivyo na msingi katika biashara ya mazao yote ndani ya nchi viondolewe.
Wafanyabiashara wa ndani wapewe motisha wa kuwekeza katika ununuzi wa nafaka toka maeneo yenye ziada na kuuza kwenye maeneo yenye upungufu. Sera za serikali katika mazao ya chakula hazitabiriki. Wakuu wa Wilaya wanaweza kuzuia uuzaji wa nafaka nje ya wilaya zao. Matokeo yake hakuna wafanyabiashara wa nafaka inayozalishwa nchini wenye mtazamo wa muda mrefu badala yake kuna walanguzi wenye mtazamo wa muda mfupi.
Hivi sasa serikali ianze uhamasishaji wa uzalishaji wa mazao yanayokomaa kwa muda mfupi katika maeneo yanayopata mvua za vuli. Utaratibu mzuri wa usambazaji wa mbegu bora, mbolea na pembejeo unahitajika. Usambazaji wa vocha za mbolea umejaa ufisadi. Mbolea inachakachuliwa na haikidhi viwango na kuwapa hasara wakulima.
Wakuu wengi wa wilaya wameteuliwa kwa upendeleo wa kisiasa na hisia binafsi na hawana uwezo wa kusimamia maendeleo ya kilimo. Badala yake Wakuu wa wilaya ni vikwazo vya maendeleo ya kilimo. Wanatoa maagizo na amri zinazowakwaza wakulima. Uteuzi wa Wakuu wa wilaya na wa mikoa uzingatie uwezo wa kuongoza na kusimamia maendeleo ya kilimo.
 Sera ya Kilimo Kwanza imejikita katika kuwatumia wakulima wakubwa kuwaendeleza wakulima wadogo wadogo. Hii ni ndoto ya Alnacha. Wakulima wakubwa wanahitaji ardhi na vibarua. Maslahi ya wakulima wakubwa yanakinzana na maslahi ya wakulima wadogo wadogo. Kwa kuwa tuna ardhi ya kutosha wakulima wakubwa wenye mitaji wana nafasi katika kukuza kilimo cha Tanzania lakini wasitegemewe kuwa ndiyo chachu ya kuwaendeleza wakulima wadogo wadogo. Sera muafaka kwa Tanzania ni kuhakikisha kuwa wakulima wadogo wadogo wanashiriki katika kilimo cha biashara cha kuzalisha mazao ya ziada na kuyauza kwenye soko. Mafunzo kwa wakulima na huduma za ugani kuhusu kilimo cha kisasa ni muhimu sana. Taaluma ya ubwana na ubibi shamba irejeshewe hadhi yake na wataalam wa kilimo wapewe motisha ya kufanya kazi yao. Wakulima wapate pembejeo ikiwa ni pamoja na mbegu bora na mbolea, na zana za kilimo.
Ile ahadi ya serikali za nchi za nchi za SADC ya kutumia alau asilimia 10 ya bajeti ya serikali katika sekta ya kilimo itekelezwe. Maeneo muhimu ya kuwekeza ni pamoja na utafiti wa kilimo, barabara za vijijini na mawasiliano, mfumo wa kilimo cha umwagiliaji maji, usambazaji wa pembejeo, huduma za fedha za kuweka akiba na kukopa kununulia pembejeo.
Tanzania ina fursa ya kukuza sekta ya kilimo kwa wastani wa asilimia 8 kwa mwaka kwa muda ya miaka 10 ijayo ukilinganisha na ukuaji wa wastani wa asilimia 4 katika miaka 10 iliyopita . Tuna ardhi ya kutosha kukidhi mahitaji yetu ya chakula na kuuza nchi za nje. Sekta ya kilimo inapokua kwa kasi inachochea ukuaji wa sekta nyingine. Upatikanaji wa chakula kwa bei nafuu unapunguza gharama za maisha na gharama za kuajiri wafanyakazi wenye afya njema. Kilimo cha kisasa kinahitaji mbolea, mbegu bora na utaalamu. Gesi iliyonguduliwa inaweza kutumiwa kutengeneza mbolea. Kilimo kinahitaji huduma za usafiri – kusafirisha pembejeo na mazao ambao unaongeza ajira. Mazao ya kilimo ni malighafi katika viwanda vya kusindika nafaka, matunda, maziwa na nyama. Viwanda vya nguo na bidhaa za ngozi vinatumia malighafi inayozalishwa na kilimo. Kipato cha wakulima kinapoongezeka wananunua bidhaa za viwandani kama vile nguo, vyombo vya nyumbani, samani, mabati, saruji na vifaa vinginevyo. Mapinduzi ya kilimo yatachochea ukuaji wa sekta ya viwanda na kuongeza ajira katika sekta rasmi.
Ili kuasisi mapinduzi endelevu ya kilimo yatakayomsaidia mkulima wa kawaida Tanzania inahitaji uongozi wenye dira. Serikali ya CCM imewasaliti wakulima wa Tanzania na kuwaongezea umaskini. Jukumu muhimu la wanaharakati wa dira ya mabadiliko ni kuwaelimisha na kuwahamasisha wakulima washiriki kikamilifu katika mabadiliko ya kisiasa yatakayoasisi mapinduzi ya kilimo yatakayowanufaisha Watanzania wote.







No comments:

Post a Comment