Tuesday, November 6, 2012

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU JUHUDI ZA CUF ZA KUENDELEZA AMANI NA UTULIVU BAADA YA SALA YA IJUMAA TAREHE

Mwenyekiti Cuf Taifa - Prof Ibrahim Haruna Lipumba
THE CIVIC UNITED FRONT
(CUF – Chama Cha Wananchi)
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU JUHUDI ZA CUF ZA KUENDELEZA AMANI NA UTULIVU BAADA YA SALA YA IJUMAA TAREHE 2 NOVEMBA 2012
Siku ya Alhamis nikielekea Muhimbili kumpeleka shangazi yangu hospitali nilipata taarifa kuwa Imam wa msikiti wa Masjid Haq (ulioko jirani na Afisi Kuu ya CUF na ambapo nasali sala ya Ijumaa nikiwa Afisi Kuu) na watu wengine watatu akiwemo Sheikh Ramadhan S. Sanze (ambaye namfahamu kwa muda mrefu). Sadik Gogo na Mzee Abdillah wamekamatwa na wamefikishwa kituo cha polisi cha kati (Central Police Station). Nilistushwa na kamata kamata hii na nikahofia kuwa inaweza kuongeza jazba miongoni mwa waumini wa Kiislam. Baada ya shangazi kupata tiba katika hospitali ya Muhimbili nilimrudisha nyumbani na nikampigia simu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na mahusiano ya umma, Abdul Kambaya, tukutane kituo cha polisi cha kati kuulizia sababu za kukamatwa Imam wa Masjid Haq na wenzake watatu na kama tunaweza kuwawekea dhamana.
Tulipofika kituo cha polisi tulibaini kuwa Imam wa Msikiti wa Masjid Haq hajakamatwa bali kuna muumini mwingine kwa jina la Mkadam Swalehe ndiye aliyekamatwa. Tulizungumza na RPC Kova na RCO Msangi kuhusu kuachiliwa kwa wale waliokamatwa. Tukafahamishwa kuwa itabidi wafanyiwe mahojiano na baadaye wataachiliwa isipokuwa Mkadam Swalehe ambaye ana faili jingine pale polisi linaloendelea kufanyiwa upelelezi. Tulifahamishwa kuwa nitume mtu saa 10:30 jioni ili aweze kufuatilia utaratibu wa kuachiliwa watuhumiwa watatu akiwemo Sheikh Ramadhan Sanze, Sadik Gogo na Mzee Abdillah.
Nilishauriana na Wakurugenzi wa CUF walioko Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu, Julius Mtatiro hatua za kuchukua. Taarifa za kukamatwa Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake zilikuwa zinaenea na kupandisha jazba ya Waislam wengi. Tulipata wasiwasi kuwa jazba hii inaweza kupelekea Waislam wengi kuandamana baada ya sala ya Ijumaa. Ikiwa Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake wataachiwa na Waislam wakapata taarifa hiyo inaweza kusaidia kupunguza jazba na watu wasishiriki maandamano baada ya sala ya Ijumaa.
Nilimpa jukum Abdul Kambaya afuatilie Central PoliceStation, suala la kuachiliwa Sheikh Sanze na wenzake. Niliwasiliana naye kwa simu na kuzungumza na RCO na nikaamini kuwa Sheikh Ramadhan Sanze, Sadik Gogo na Mzee Abdillah wataachiwa baada ya kukamilisha mahojiano. Ilikuwa inakaribia saa 12 jioni. Muda wa kuitisha Press Conference haukuwepo. Tukakubaliana Naibu Katibu Mkuu awasiliane na wahariri wa habari wa vituo vya televisheni Channel 10, TBC1, Star TV, Mlimani TV na ITV ili niweze kutoa taarifa ya kuwasihi Waislam warudi majumbani na kwenye shughuli zao baada ya sala ya Ijumaa. Niliweza kufanya mahojiano na Channel 10, TBC1, na ITV. Kwa bahati mbaya Camera person wa Star TV alikuwa kwenye shughuli nyingine na kwa hiyo sikuweza kufanya mahojiano na Star TV. Vilevile wapiga picha wa Mlimani TV hawakuwepo kwenye studio. Pia nilipata bahati ya kuzungumza na Radio Iman inayosikilizwa na Waislam wengi na kueleza maoni yangu kuwa Waislam wasiandamane baada ya sala ya Ijumaa.
Baada ya kutoa taarifa kwenye vituo vitatu vya televisheni na Radio Iman kuwa Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake wataachiliwa na kuwasihi Waislam wasishiriki maandamano baada ya sala ya Ijumaa nilimpigia simu Abdul Kambaya kuulizia kama naweza kuzungumza na Sheikh Ramadhan Sanze. Kambaya akanieleza mambo yamebadilika na hawajaachiwa. Niliwasiliana na RCO na nikabaini kuwa suala hilo haliko tena chini ya uamuzi wake na litakamilishwa siku ijayo.
Usiku wa alhamisi kuamkia Ijumaa nilijaribu kuwasiliana na Rais Kikwete kupitia wasaidizi wake ili nimfahamishe mantiki na sababu ya hatua nilizochukua na atumie uwezo wake alionao Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake waachiliwe. Kwa bahati msaidizi mmoja alipata ujumbe wangu wa simu na akanipigia simu saa 6:50 usiku na kunifahamisha atajitahidi kuufikisha ujumbe wangu kwa Mhe. Rais ili nipate kuongea naye kuhusu jamaa wanaoshikiliwa na polisi waachiwe ili kupunguza jazba na kuepusha shari. Niliyezungumza naye alikuwa Dodoma na Rais alikuwa Arusha na ratiba yake ilikuwa imebana sana na kwa hiyo hakuweza kupata fursa ya kunipigia simu siku hiyo ya Ijumaa.
Siku ya Ijumaa Abdul Kambaya aliendelea kufuatilia kuachiwa kwa Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake Central Police Station. Nami katika kuhangaika ili waliokamatwa waachiliwe nilipata fursa ya kuzungumza na IGP na kumfahamisha sababu ya juhudi nilizochukua na mategemeo yangu kuwa Sheikh Sanze na wenzake wangeachiwa. Ninakiri kuwa katika mazungumzo ya simu, IGP Mwema alikuwa msikivu na mkarimu sana katika kauli yake. Alinishukuru kwa kauli niliyoitoa katika vituo vya televisheni na kuwa atafuatilia suala nililomueleza. Hatimaye Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake waliachiwa.
Naamini kama Sheikh Ramadhan Sanze na wenzake wangeachiwa ingesaidia sana kupunguza jazba. Hata hivyo Waislam wengi na wananchi wengine kwa ujumla walipokea vizuri wito wangu na hawakushiriki katika maandamano. Baadhi wamenikosoa na kushauri kuwa ilifaa nisubiri mpaka baada ya maandamano kufanyika na kama patatokea majeruhi na vifo ndipo nitoe tamko la kulaani vitendo vya polisi na serikali.
Katika mitandao ya kijamii wengine wamekejeli juhudi zangu. Nilikubali kushiriki katika kipindi cha Makutano show kinachoendeshwa na Bi. Fina ambapo hupata maswali toka Jamii Forum. Moja ya swali lililotolewa ni “Muulize very very solid, kuna agenda gani kati ya Cuf na uislam? mtaani leo wanasema kauli ya Lipumba ya jana kusitisha maandamano wameitii, na ukiangalia mikutano yake pale jangwani utafikiri kuna mawaidha ni balaghashia na baibui.” Fina hakupata muda wa kuniuliza swali hili. Jibu lake ni la wazi. CUF inasimamia Haki Sawa kwa Wananchi Wote. Kuna Watanzania wengi ambao ni Waislam na wao pia wanastahiki kutendewa haki katika nchi yao. Kuhusu balaghashia na baibui ni vyema vijana wakatazama picha za umati wa watu uliokuwa unahutubiwa na Mwalimu Nyerere wakati wa kupigania uhuru wa nchi hii. Picha hizo pia zinaonyesha waliokuwa wakipigania uhuru wengi walivaa balaghashia na baibui hata Mwalimu Nyerere alipewa zawadi nyingi za balaghashia na akaamua kuzivaa.
Kushamiri kwa demokrasia ya kweli msingi wake mkubwa ni amani na utulivu. Amani ya kweli haipatikani bila kuwepo haki. Kesi ya Sheikh Ponda msingi wake na madai ya kiwanja. Ki msingi kesi ya madai ya kusuluhishwa na Mahakama ya ardhi. Sheikh Ponda ana haki ya msingi ya kupewa dhamana hata kama kauli zake haziifurahishi serikali.
Nasikitika sana katika kipindi hiki tete, viongozi wa serikali wameshindwa kuchukua juhudi za makusudi kuzungumza na Maimam wa misikiti na viongozi wa asasi za Kiislam kupunguza jazba. Badala yake wameachia kauli za vitisho vya Kamanda Kova ndiyo viwe mawasiliano kati ya serikali na Waislam. Ni vyema serikali ikatumia busara na kuwasiliana na Maimamu wa misikiti na viongozi wa asasi za Kiislam kuelewa hoja na malalamiko yao.
Hatimaye nimepata fursa ya kuzungumza na Mheshimiwa Rais leo asubuhi na nikamueleza juhudi nilizozichukua kuweza kupunguza jazba na kuwaomba Waislam wasishiriki kwenye maandamano baada ya sala ya Ijumaa. Ni wazi hali hii ya mtafaruku ndani ya jamii inamsononesha sana Mheshimiwa Rais na ninaamini atajitahidi kwa uwezo wake wote kutafuta suluhisho.
Katika kutafuta suluhu ya mtafaruku huu nitaendelea na jitihada za kutafuta fursa niweze kubadilishana mawazo na Rais Kikwete. Nitazungumza na viongozi wa asasi za Kiislam. Nitazungumza na viongozi wa Makanisa ya Kikristo. Madhumuni ya mazungumzo yangu ni kuwafahamisha mantiki ya juhudi nilizofanya na kushauriana misingi muhimu ya Waumini wote kuheshimiana na kuvumiliana ili tujenge Tanzania yenye haki sawa kwa wote.

Ibrahim Haruna Lipumba
Mwenyekiti
Novemba 4 2012

No comments:

Post a Comment