Tuesday, September 4, 2012

Kodi, Utawala bora na Maendeleo ya Taifa


Prof Ibrahim Lipumba
Mwenyekiti Wa Cuf Taifa
Katika nchi nyingi maskini, mipango na miradi ya maendeleo na usambazaji wa huduma za msingi unakwamishwa na serikali isiyokuwa na fedha za kutosha. Katika kusimamia maendeleo hakuna sera muhimu ya serikali inayozidi mfumo na viwango vya kodi. Hata hivyo kurekebisha mfumo na kuongeza viwango vya kodi kunaweza kusababisha serikali kuanguka. Matumizi ya serikali yanahitajika katika kuhakikisha kuwepo kwa amani, utulivu na usalama wa raia. Huduma za msingi za jamii kama vile elimu bora kwa watoto wote, huduma za afya za msingi kwa wananchi zinahitajika ili wananchi wafurahie maisha yao lakini vile vile wananchi wenye elimu na afya bora wanakuwa na tija kubwa katika uzalishaji wa bidhaa na huduma. Kukuza uchumi utakaowaletea neema wananchi wote kunahitaji miundombinu ya barabara, reli, bandari, viwanja vya ndege, ufuaji na usambazaji wa umeme, utafiti wa kilimo na huduma za ugani. Katika maeneo mengi ya miundimbinu, sekta binafsi haiwezi kuwekeza. Serikali ina jukumu la kuendeleza miundombinu na kusambaza huduma za jamii.
Kwa muda mrefu bajeti ya Tanzania imetegemea kwa kiwango kikubwa cha asilimia 30-40 fedha kutoka kwa wahisani wa nchi za nje. Ukusanyaji wa mapato ya ndani umeongezeka. Lakini nakisi ya bajeti ya serikali pia imekuwa inaongezeka mpaka kufikia zaidi ya asilimia 11 katika miaka mitatu ya fedha 2009/10 – 2011/12. Katika miaka ya fedha 15 iliyopita mapato ya ndani hayakidhi matumizi ya kawaida. Kwa hiyo mapato ya kodi hayachangii bajeti ya maendeleo. Tanzania inahitaji iongeze ukusanyaji wa kodi ufikie asilimia 22 – 25 ya pato la taifa ukilinganisha na ukusanyaji wa mapato ya ndani ya asilimi 16 hivi sasa.
Mchakato wa ujenzi na uimarishaji wa dola unaenda sambamba na uwezo wa serikali kukusanya kodi na mapato mengine. Ulipaji na ukusanyaji wa kodi na usambazaji wa huduma za serikali unatoa fursa ya ujenzi wa uhalali wa dola katika jamii. Ikiwa ukusanyaji wa kodi ni wa kutumia mabavu na kuwanyanyasa wananchi kama ilivyokuwa katika ukusanyaji wa kodi ya kichwa wakati wa ukoloni ambayo baada ya uhuru ilibatizwa jina zuri na kuitwa kodi ya maendeleo, uhalali wa dola unaathirika na mahusiano ya dola na raia yanakuwa mabovu. Ikiwa mfumo na viwango vya kodi vinatokana na majadiliano na makubaliano kati ya serikali na wananchi, ulipaji na ukusanyaji wa kodi una fursa ya kuchangia katika ujenzi wa dola yenye uhalali mbele ya jamii. Mapinduzi ya Marekani ya mwaka 1776 yalianza kama mgomo wa kulipa kodi kwa serikali ya Mfalme wa Uingereza. Kauli mbiu ya Wamarekani ilikuwa “No taxation without representation” tafsiri yake ikiwa hakuna kulipa kodi bila kuwakilishwa.
Sera za kodi zinapaswa kutazamwa na kuchambuliwa kwa upana zaidi. Ulipaji na ukusanyaji kodi uwe nyezo ya kujenga dola yenye uhalali na inayowajibika kwa wananchi. Ili azma hii ya ujenzi wa dola yenye uhalali iweze kufikiwa ni lazima mfumo wa kodi uwe na uonekane kuwa ni wa haki na unaendeleza usawa katika jamii. Matumizi ya serikali yawe adilifu na wananchi waone wananufaika na kodi wanazolipa. Ikiwa kazi kubwa ya polisi ni kupokea rushwa na kuwabambikizia kesi wananchi, majambazi yanawapora wananchi, hakuna usalama wa raia na mali zao, mahakama zimejaa rushwa, huduma za afya mbovu, watoto hawapati elimu bora, barabara hazitengenezwi, umeme unakatika kila wakati ni vigumu kuwahamasisha wananchi kulipa kodi na kutumia mfumo wa kodi kujenga dola yenye uhalali kwa wananchi.
Watanzania wengi wanaamini kuwa mfumo wa kodi hauna haki na unawabana wananchi maskini. Theluthi moja ya mapato ya kodi inatokana na kodi ya ongezeko la thamani (VAT) ambayo kila mnunuzi wa bidhaa na huduma analipa kiwango sawa cha kodi bila kujali kama ana kipato kikubwa au kidogo. Makampuni makubwa na hususan makampuni ya madini yamepewa misamaha ya kodi. Wawekezaji wa nje wanasamehewa kodi lakini makampuni ya ndani yanabanwa kulipa kodi. Mawaziri, Wabunge, Maafisa waandamizi katika serikali na mashirika ya umma wanasamehewa kodi wanapoagiza magari na vifaa vingine kutoka nje.
Ili kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari na kuongeza mapato ya serikali ni lazima kurekebisha mfumo wa kodi uwe wa haki na usawa. Wananchi washirikishwe kwa kupewa elimu ya kweli kuhusu mfumo wa kodi. Mijadala kuhusu mfumo wa kodi iwe wazi.
Kuwepo kwa utamaduni mzuri wa kulipa kodi unamfanya mwananchi aone fahari kulipa kodi kwa mujibu wa sheria zilizopo. Ulipaji kodi wa hiari unategemea sana imani ya walipa kodi kuhusu mfumo mzima wa kodi na jinsi mamalaka ya kodi inavyotekeleza wajibu wake. Ulipaji wa kodi wa hiari unakuwepo ikiwa wananchi wanahisi kuwa kama raia wana wajibu wa kulipa kodi. Kuwa na hisia kuwa kulipa kodi ni wajibu kanategemea sana wananchi kuamini kuwa serikali inatumia vizuri na kwa uadilifu fedha za kodi kwa manufaa ya umma.
Utendaji ulio wazi na wa haki wa wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato unasaidia sana katika kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari. Ikiwa jamii inaamini kuwa rushwa imekithiri katika mamlaka ya mapato, utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari hauwezi kujengeka. Kuongeza uwezo na nguvu za mamlaka ya mapato zinaweza kusaidia zaidi kuongeza mapato ya wakusanya kodi kuliko mapato ya serikali. Katika kuandaa na kutekeleza sera za kodi ni muhimu kuzingatia hali halisi ya uchumi na jamii ya nchi husika. Sera za kodi za nchi zilizoendelea zinasisitiza sana ufanisi katika mfumo, viwango na ukusanyaji wa kodi. Pia huzungumzia masuala ya kukwepa kulipa kodi lakini mara nyingi hawachambui matatizo ya rushwa katika ulipaji na ukusanyaji wa kodi. Tatizo la kukabiliana na rushwa linapaswa kuzingatiwa kwa makini katika kuandaa na kutekeleza sera za kodi. Mfumo wa kodi unaofaa kwa nchi nyingi zinazoendelea kama Tanzania ni ule utakaopunguza mianya ya rushwa.
Viwango vya kodi vinaweza kukwaza ilipaji wa kodi wa hiari. Mzigo wa kodi ukiwa mkubwa sana watu watakwepa kulipa kodi. Ikiwa utaratibu wa kulipa kodi ni mwepesi na hauna gharama kubwa ya muda na pesa, ulipaji wa kodi wa hiari utaongezeka. Kama kuna watu wengi na kampuni nyingi zinazokwepa kulipa kodi, zitawakatisha tamaa wale wanaolipa kodi kwa hiari. Kuwepo kwa ukwepaji kodi ambao hauadhibiwi kunaongeza ukwepaji kodi. Kama wananchi wanaamini kuwa hakuna ukwepaji wa kodi mkubwa, wengi watajitokeza kulipa kodi.
Maeneo muhimu ya kuimarisha ulipaji wa kodi wa hiari ni pamoja na sera za kodi, utawala na uendeshaji wa mamlaka ya kukusanya mapato na uadilifu katika matumizi ya fedha za umma.
Sera za kodi zinapaswa kuwa wazi, nyepesi kuzielewa na zisimamie haki na usawa. Viwango vya kodi viwe vya wastani na vichache. Changamoto kubwa inayoathiri ujenzi wa mfumo wa kodi ulio na uwazi na unaowajibika kwa jamii ni misamaha ya kodi kwa wawekezaji wa nje. Misamaha ya kodi inapunguza mapato na kuchochea rushwa na ukwepaji wa kodi. Likizo za kodi ya mapato ya wawekezaji wa nje zinatumiwa vibaya kujenga utaratibu wa kuongeza gharama za uendeshaji ili kupunguza faida na kwa hiyo kulipa kodi kidogo. Kwa mfano makampuni binafsi ya usafiri wa ndege yalikopa katika benki za hapa hapa nchini kununua ndege za abiria. Baada ya kumaliza kulipia mkopo, walihamisha usajili wa ndege hizo kwenda Cyprus haidhuru ndege zimenunuliwa hapa hapa na zipo nchini. Sasa makampuni haya yanaandaa hesabu za mapato na matumizi zinazoonyesha kuwa  wamekodisha ndege toka Cyprus na kwa hiyo wanalipa ada ya kukodisha na kupunguza faida wanayopata na kodi ya mapato wanayolipa. Vitendo kama vinaendelea kufanyika kwa sababu ya kuwepo rushwa ndani ya mamlaka zinazosimamia usafiri wa anga na ukusanyaji wa kodi.
Watanzania wengi wanaamini kuwa mfumo wa kodi hauna haki unapendelea wawekezaji wa nje. Katika mazingira haya ni vigumu kujenga utamaduni wa kulipa kodi kwa hiari. Kufuta misamaha ya kodi ni hatua muhimu katika kuhamasisha ulipaji wa kodi wa hiari na kuishirikisha wananchi katika mijadala ya kodi itakayosaidia kujenga jamii itakayokuwa na fahari katika ulipaji wa kodi.
Mamlaka ya mapato ina kazi muhimu tatu. Mosi kujenga utaratibu rahisi wa kulipa kodi. Pili, kufuatilia na kuhakikisha kuwa wahusika wote wanalipa kodi zinazowahusu na wale wanaokwepa kulipa kodi wanachukuliwa hatua za kisheria. Tatu kuboresha utaratibu wa kulipa kodi ili wananchi wengi walipe kodi kwa hiari. Mamlaka ya mapato ina wajibu wa kujenga mazingira ya kurahisha ulipaji wa kodi na iwe na ufuatiliaji makini wa kuhakikisha kodi zinalipwa na wanaokwepa wanaadhibiwa kwa mujibu wa sheria.
Ili wananchi wajue wajibu wao wa kulipa kodi, elimu ya uraia kuhusu kodi ni muhimu. Kwa wananchi wa kawaida katika sekta isiyo rasmi ni vizuri elimu kuhusu kodi iambatane na mafunzo ya ujasiriamali na uendeshaji wa shughuli za biashara. Huduma kwa walipa kodi zihakikishe kuwa utaratibu wa kulipa kodi unakuwa mwepesi. Gharama za kukwepa kodi kwa maksudi ziwe kubwa ili wananchi wawe na motisha wa kulipa kodi. Wanaolipa kodi kwa hiari wataongezeka ikiwa maafisa wa Mamalaka ya Mapato itawaheshimu na kuwatendea haki bila upendeleo kwa baadhi ya walipa kodi. Vitendo vya ufisadi vya baadhi ya maafisa wa Mamlaka ya Mapato ya kuwabana wafanyabiashara watoe rushwa ili wasiongezewe kodi vinaathiri sana ujenzi wa utamaduni wa kulipa kodi.
Ni muhimu kuwepo na uhusiano wa karibu na unaoonekana kati ya kulipa kodi na huduma za serikali. Uadilifu katika matumizi ya serikali na huduma bora zinazogharimiwa na serikali zinasaidia kuongeza motisha wa kulipa kodi. Kwa mfano serikali iwe wazi katika kuonyesha ujenzi na ukarabati wa barabara unaolipiwa na kodi ya mafuta ya petroli kwa ajili ya kujenga barabara.
Watanzania wengi hawashiriki katika kulipa kodi ya mapato. Katika nchi yenye watu milioni 44, ni wananchi laki tano tu ndiyo wenye namba za kulipia kodi. Wananchi wengi wameajiriwa au kujiajiri katika sekta ya kilimo asilia vijijini na sekta isiyo rasmi. Baadhi ya wananchi katika sekta isiyo rasmi wana vipato vikubwa vya kuweza kulipa kodi. Kuzirasimisha shughuli za sekta isiyo rasmi kuna faida kwa wajasiriamali wa sekta hiyo. Shughuli zao zinapofahamika wanaweza kupata mikopo ya kupanua biashara zao, mafunzo ya ujasiriamali, masoko na teknolojia bora ya kuendeleza shughuli zao. Mkakati wa kupanua wigo wa walipa kodi toka sekta isiyo rasmi ujikite katika mafunzo ya ujasiriamali yatakayoongeza ufanisi na faida kwa wafanya biashara wa sekta isiyo rasmi na kuwawezesha kulipa kodi bila kuathiri sana mapato yao.
Athari kwa utawala bora kwa nchi inayotegemea wigo mkubwa wa walipa kodi na uwezo wa serikali kukusanya kodi ni pamoja na kuwa na dola inayowajibika katika matumizi ya fedha za walipa kodi kuhakikisha inawaletea neema wananchi wake wote. Ili serikali ikusanye kodi za kutosha toka kwa wananchi inabidi ijenge uwezo wa kupata taarifa ya mapato na matumizi ya raia ili kuweza kukusanya kodi kwa ufanisi na uadilifu. Juhudi za kujenga uwezo wa kukusanya kodi zinaifanya serikali kwa ujumla wake kuwa na uwezo wa kiutawala.
Raia wanaotozwa kodi wanakuwa na shauku ya kujua matumizi ya kodi zao na kwa hiyo kuishinikiza serikali kuwajibika katika matumizi yake. Mchakato wa kutoza na kukusanya kodi unawafanya raia kuafiki kulipa kodi kwa hiari ikiwa wanaamini kodi zao zinatumiwa vizuri kwa manufaa ya umma. Viwango vya kodi visiwe vya juu sana vinavyoathiri vibaya maisha ya mlipa kodi. Kushiriki kwa wananchi katika mijadala ya sera za kodi na matumizi ya serikali kunasaidia kuweka viwango na mfumo wa kodi unaotabirika. Bunge linapata nguvu ya kuiwajibisha serikali.
Bila kuweka utaratibu wa mkataba wa jamii (social contract) kati ya wananchi na dola kupitia ulipaji kodi, wananchi hawawezi kuwa na motisha wa kujenga uwezo wa kuchunguza na kukagua matumizi ya serikali na kuiwajibisha. Bila wananchi kuwa ngangari wa kujua matumizi ya fedha zao za kodi, hapawezi kuwepo na ufanisi wa kutosha katika matumizi ya serikali.
Wananchi watakuwa na motisha kufuatilia ufanisi wa matumizi ya serikali ikiwa kwa kiasi kikubwa matumizi hayo yanatokana na ulipaji wa kodi wa wananchi wenyewe na siyo misaada kutoka nje. Kuendelea kutegemea misaada ya nje kunaathiri kujenga dola inayowajibika kwa wananchi. CCM imejenga dola tegemezi. Ni muhimu kwa Watanzania kujipanga na kuchagua uongozi wenye dira utakaouhakikisha kuwa misamaha holela ya kodi inaondolewa, wawekezaji wa nje wanalipa kodi, mfumo wa kodi unakuwa wa haki sawa kwa wote na utaratibu wa kulipa kodi unaasisi mkataba wa jamii wa kuiwajibisha serikali na kuhakikisha matumizi ya serikali yanaelekezwa kukidhi mahitaji ya wananchi na kuchochea maendeleo.



No comments:

Post a Comment