Sunday, September 16, 2012

TANZANIA TUKO NYUMA SANA KATIKA USHINDANI WA KIUCHUMI WA KIMATAIFA

Mwenyekiti Cuf Taifa- Prof Ibrahim Lipumba

Taarifa ya kila mwaka inayotolewa na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya World Economic Forum (WEF) kuhusu ushindani wa kiuchumi wa mataifa(The Global Competitiveness Report 2012/13) inaonesha kuwa Tanzania imeshika nafasi ya 120 kati ya nchi 144 wakati nchi jirani ya Rwanda imeshika nafasi ya 63.
Nchi inayoongoza kwa ushindani wa kiuchumi wa mataifa ni Uswissi (Switzerland), ikifuatiwa na Singapore, Finland, Uswidi (Sweden), Uholanzi (Netherlands), Ujerumani, Marekani, Uingereza, Hongkong na Japan.
Katika nchi za Afrika inayoongoza kwa ushindani wa kiuchumi ni Afrika ya Kusini inayoshika namba ya 52, ikifuatiwa na Mauritius ambayo ni ya 54 na ya tatu ni Rwanda iliyoshika nafasi ya 63 katika orodha ya nchi 144.
Watafiti wa WEF wanaeleza kuwa ushindani wa uchumi wa taifa unatokana na asasi za uchumi na utawala, sera, raslimali na nguvukazi (raslimali watu) zinazobainisha kiwango cha tija katika uzalishaji wa bidhaa na huduma katika nchi na kwa hiyo kuiwezesha nchi kukuza uchumi kwa kasi, kuongeza utajiri wa nchi na neema kwa wananchi wake.
Ili kupima ushindani wa kiuchumi wa kila nchi, watafiti wamechunguza mambo ya msingi yanayochochea ukuaji wa uchumi na uletaji wa maendeleo kwa ujumla. Nchi zenye ushindani wa kiuchumi zinafanikiwa kuongeza ufanisi na tija katika uzalishaji wa bidhaa na usambazaji wa huduma. Zinatumia vizuri raslimali na nguvukazi na kwa hiyo kufanikiwa kukuza uchumi kwa muda mrefu. Katika ulimwengu wa utandawazi ambapo nchi zina fursa ya kuuza na kununua bidhaa na huduma katika soko la dunia ushindani wa kiuchumi ni nyenzo muhimu ya kuongeza kasi ya kukuza uchumi kwa kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.
Watafiti wa WEF wanaanda kielelezo (farihisi) cha ushindani wa uchumi wa mataifa. Kielelezo hiki kutunamia vigezo vingi kupima ushindani wa kiuchumi unaotokana na asasi, sera, raslimali na vipengele vingine ambavyo vinabainisha uwezo, ufanisi na kiwango cha tija katika uzalishaji mali wa sekta mbali mbali za uchumi na huduma. Kiwango cha tija na ufanisi katika uzalishaji ndicho kinachovutia uwekezaji wa ndani na nje na kuchochochea ukuaji wa uchumi na ongezeko la wastani la pato la kila mwananchi.
Utafiti wa WEF umebaini nguzo 12 za ushindani wa kiuchumi wa mataifa. Nguzo ya kwanza ni asasi za uchumi, utawala na sheria ambazo zinajenga mazingira ya kushirikiana katika shughuli za kiuchumi kwa mtu mmoja mmoja, kampuni na serikali katika shughuli za uzalishaji na kuongeza utajiri wa taifa. Umuhimu wa mfumo wa asasi ulio wazi na kufanya kazi kwa ufanisi na haki umebainika hata kwa nchi zilizoendelea baada ya mtikisiko na mgogoro wa sekta ya fedha ulioanza Marekani mwaka 2008 na kuikumba dunia yote. Ukosefu na udhaifu wa usimamizi wa asasi za fedha katika nchi zilizoendelea na hasa Marekani ndiyo chanzo cha kuporomoka na kuyumba kwa uchumi wa dunia kwa muda wa miaka minne iliyopita.
Ubora wa asasi za uchumi na utawala ni jambo la msingi katika ushindani wa kiuchumi wa kila taifa. Mfumo na utendaji wa asasi hizi ndiyo unaoshawishi uwekezaji wa vitega uchumi na uzalishaji wa bidhaa na huduma. Mfumo wa asasi ndiyo kigezo muhimu cha mgawanyo wa pato la taifa na gharama za utekeleza wa mikakati ya kukuza uchumi. Kwa mfano kuwepo kwa hakimiliki za kuaminika ni muhimu sana katika kushawishi uwekezaji. Ikiwa mali ya mtu inaweza kuporwa kwaurahisi na watu wengine au serikali, uwekezaji wa vitega uchumi utapungua.
Ubora wa mfumo wa asasi ni pamoja na kuwepo utawala bora, ufanisi katika shughuli na usambazaji wa huduma za serikali, kutokuwepo kwa rushwa, ukusanyaji mzuri wa kodi na uadilifu katika matumizi ya fedha za umma. Utendaji, ufanisi na maadili ya sekta binafsi yanachangia katika kujenga ushindani wa kiuchumi wa taifa husika.
Nguzo ya pili ya ushindani wa kiuchumi ni miundombinu. Miundombinu inayojumlisha usafiri- barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege; ufuaji na usambazaji wa umeme; ugawaji na usambazaji wa maji; miundombinu ya majitaka, na miundombinu ya mawasiliano inayoharikisha upeanaji wa taarifa na habari. Ubora wa miundombinu unachangia sana katika kuongeza ufanisi na tija ili kukuza uzalishaji na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Nguzo ya tatu ni utengamavu wa uchumi mpana (macroeconomic stability) kwa maana ya mfumko wa bei wa kadri, riba ziwe za nafuu na pasiwe na tofauti kubwa sana kati ya riba ya mikopo na riba wanaolipwa waweka akiba,  thamani ya sarafu iwe tengamavu na ya ushindani kwa wazalishaji wa bidhaa na huduma wa ndani ya nchi, akiba ya kutosha ya fedha za kigeni ya kuagizia bidhaa na huduma za nje, matumizi ya serikali yasizidi mapato ya serikali kwa kiasi kikubwa. Utengamavu wa uchumi mpana pekee haukuzi uchumi, bali unajenga mazingira ya kuvutia uwekezaji na ukuaji wa uchumi ikiwa mambo mengine kama vile miundombinu na asasi bora vipo. Kutokuwepo kwa utengamavu wa uchumi mpana kunaathiri motisha wa uwekezaji na uzalishaji kwani kunaweka mashaka makubwa kwa bei halisi za raslimali, nguvukazi, bidhaa na huduma mbalimbali.
Nguzo ya nne ni afya na elimu bora ya msingi. Wananchi wenye afya njema wana uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi na tija ya juu. Wananchi weye afya mbovu siyo wazalishaji wazuri. Afya duni inaongeza gharama za uzalishaji. Ubora wa elimu ya msingi kwa wananchi wote inawezesha wafanyakazi waweze kufundishika. Wafanyakazi wasiokuwa na elimu bora ya msingi na kujua kusoma vizuri siyo wepesi kujifunza teknolojia mpya ya uzalishaji.
Nguzo ya tano ni elimu na mafunzo ya juu. Elimu bora ya juu na hususan elimu ya sayansi na teknolojia ni muhimu kwa nchi zinazohitaji kuzalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na bidhaa za teknolojia. Katika ulimwengu wa utandawazi , kuwa na watu wenye elimu ya juu ya sayansi na teknolojia ni muhimu katika kujenga ushindani wa uzalishaji wa bidhaa za kisasa.
Nguzo ya sita ni ufanisi wa soko la bidhaa. Nchi zenye masoko ya bidha yenye ufanisi na ushindani halali yanavutia uwekezaji na uzalishaji wa bidhaa na huduma bora. Ushindani wa soko ni muhimu katika kumotisha uvumbuzi na ufanisi katika uzalishaji. Kodi za juu zinaondoa motisha na kuathiri ushindani wa kiuchumi. Katika soko ambalo wateja wake wana utamaduni wa kutaka bidhaa bora unasaidia kulazimisha kampuni zishindane katika kuzalisha bidhaa bora.
Nguzo ya saba ni ufanisi wa soko la ajira. Ufanisi na mnyumbuliko wa soko la ajira ni jambo la msingi katika kuhakikisha kuwa watu wanaajiriwa katika nyanja ambazo watakuwa na uzalishaji wenye tija kubwa kulingana na uwezo na ujuzi wao. Uchumi unaokua kwa kasi kubwa na kubadilika mfumo wake unahitaji wafanyakazi wapungue kwenye sekta zinazodidimia au kutoweka kabisa na waongezeke  katika sekta zinazokua kwa kasi. Bila kuwepo kwa mnyumbuliko wa soko la ajira, mabadiliko ya haraka ya mfumo wa uchumi kama vile kupungua kwa sekta ya kilimo na kuongezeka kwa sekta ya viwanda, hayawezi kutokea. Soko la ajira lenye ufanisi linawapa mishahara mizuri wafanyakazi hodari na makini ili kuwapa motisha wa kuendelea kuchapa kazi. Wafanyakazi wavivu na wazembe wanapata kipato kidogo ukilinganisha na wafanyakazi hodari. Wafanyakazi wote wanajua kuwa wakiendelea na uzembe watapoteza ajira.
Nguzo ya nane ni maendeleo ya soko la mitaji na huduma za fedha. Uchumi wa kisasa unahitaji huduma za mikopo na mitaji. Ukusanyaji wa akiba kwa ufanisi unaruhusu kuwepo kwa mikopo yenye riba nafuu. Akiba itumiwe vizuri kuwapa mikopo wazalishaji wenye tija ya juu. Benki na taasisi nyingine za fedha zina kazi ya kutambua wajasiriamali wenye miradi mizuri yenye tija na kuwakopesha mitaji. Kuwepo kwa benki na taasisi nyingine za fedha zinazofanya kazi kwa ufanisi kunachochea ukuaji wa uchumi.
Nguzo ya tisa ni utayari wa kiteknolojia. Katika ulimwengu wa utandawazi ambapo kuna mabadiliko ya mara kwa mara ya teknolojia ni muhimu kwa nchi kujenga uwezo wa wananchi na kampuni zilizomo nchini kupokea, kumudu na kutumia teknolojia mpya. Hivi sasa teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) imekuwa na matumizi katika nyanja zote za uzalishaji, elimu, afya na huduma nyingine. Taifa lenye miundombinu ya TEHAMA na wafanyakazi na jamii inayoweza kutumia TEHAMA ina fursa ya kuzalisha bidhaa na huduma kwa ufanisi wa juu, kuongeza tija na kukuza uchumi.
Nguzo ya kumi ni ukubwa wa soko. Ukubwa wa soko unatoa fursa kwa uzalishaji mkubwa unaopunguza wastani wa gharama za uzalishaji. Nchi zenye soko kubwa la ndani inaweza kuanzisha na kuimarisha kampuni za uzalishaji kwa kutegemea soko la ndani. Katika ulimwengu wa utandawazi, soko la dunia linatoa fursa kwa nchi ndogo, kupunguza wastani wa gharama za uzalishaji kwa kuuza bidhaa na huduma zake kwenye soko la nje ya nchi. Kwa nchi ndogo kushiriki katika soko la dunia hasa kwa kuuza bidhaa za viwandani kunaongeza kasi ya kukua kwa uchumi.
Nguzo ya 11 ni kuwepo kwa kampuni na ufanyaji biashara wa kisasa. Kampuni ndio vituo vya uzalishaji vinavyotumia teknolojia mpya kuongeza ufanisi na tija. Ubora wa mtandao wa biashara na kuwepo kwa kampuni za kisasa zenye mikakati na uendeshaji wenye ufanisi kunaongeza tija na kuchochea ukuaji wa uchumi. Nguzo hii ni muhimu zaidi kwa nchi zilizo mstari wa mbele katika maendeleo ya uchumi. Klasta (kishada) za kampuni za kisasa katika eneo moja zinasaidia sana katika uvumbuzi wa teknolojia mpya za uzalishaji wa bidhaa na usambazaji wa huduma. Klasta ya bonde la silicon (Silicon Valley), California, Marekani limechangia katika uvumbuzi mbalimbali wa TEHAMA.
Nguzo ya 12 ni uwezo wa uvumbuzi wa teknolojia mpya za uzalishaji wa bidhaa na usambazaji wa huduma. Uvumbuzi wa teknolojia mpya ndiyo unaochochea ukuaji na maendeleo ya uchumi kwa nchi zilizoko mstari wa mbele wa maendeleo kama vile Marekani, Ujerumani, Japan, Uswidi (Sweden) Uingereza, Uswissi (Switzerland) na zinginezo.
Nguzo hizi 12 za ushindani wa kiuchumi wa kimataifa zinahusiana. Nchi ikiwa dhaifu katika eneo moja basi kutakuwa na uwezekano wa kuwa dhaifu katika maeneo mengine. Kwa mfano uwezo wa uvumbuzi wa teknolojia hauwezi kuwepo bila kuwa na raslimali watu yenye afya njema na elimu nzuri na yenye uwezo wa kumudu teknolojia. Mfumo mzuri wa benki na soko la mitaji unahitajika ili kuhakikisha uvumbuzi wa teknolojia mpya yenye tija unafikishwa sokoni na kutumiwa katika uzalishaji wa bidhaa na usambazaji wa huduma.
Umuhimu wa nguzo moja moja kati ya nguzo zote 12 katika kuongeza ushindani wa kiuchumi wa mataifa na kwa hiyo kuchochea ukuaji wa uchumi unategemea hatua ya maendeleo iliyofikiwa na nchi husika. Njia bora ya Tanzania kuongeza ushindani wake wa kiuchumi siyo sawa na Uswidi kwani Tanzania ni maskini ina miundombinu mibovu na Uswidi iko mstari wa mbele katika maendeleo ya kiuchumi na teknolojia. Mishahara ya Uswidi ni ya juu wakati mishahara ya Tanzania ni ya chini na wananchi wachache sana wenye ajira za uhakika. Watanzania wengi wanategemea kilimo cha kujikimu na sekta isiyo rasmi.
Ukuaji wa uchumi katika nchi ambazo ziko chini kimaendeleo kama vile Tanzania kunategemea utumiaji wa ardhi na maliasili nyingine, na nguvukazi isiyokuwa na elimu na mafunzo ya kutosha. Kampuni zake zinashindana zaidi kwa bei za bidhaa za kawaida. Katika nchi zilizo katika hatua ya mwanzo ya maendeleo, ushindani wa kiuchumi unategemea nguzo ya kwanza ya asasi za uchumi, utawala na sheria, nguzo ya pili ya miundombinu, nguzo ya tatu ya utengamavu wa uchumi mpana (macroeconomic stability) na nguzo ya nne ya afya na elimu bora ya msingi.
Kwa kadri nchi inavyoendelea na kukamilisha matakwa ya nguzo ya kwanza mpaka ya nne ndivyo mishahara inavyoongezeka , ukuaji wa uchumi utategemea sana ongezeko la ufanisi katika uzalishaji na kuongeza ubora wa bidhaa. Katika hatua hii ya maendeleo iliyofikiwa na nchi kama Mauritius, Namibia na Afrika ya Kusini, ongezeko la tija na ukuaji wa uchumi unategemea nguzo ya tano ya elimu na mafunzo ya juu, nguzo ya sita ya ufanisi wa soko la bidhaa, nguzo ya saba ya ufanisi wa soko la ajira, nguzo ya nane ya maendeleo ya soko la mitaji na huduma za fedha, nguzo ya tisa ya utayari wa kiteknolojia, na  nguzo ya kumi ya ukubwa wa soko la ndani na uwezo wa kushindana katika soko la nje
Nchi zilizo mstari wa mbele katika maendeleo zinategemea zaidi nguzo ya 11 ya kuwepo kwa kampuni bora na ufanyaji biashara wa kisasa na nguzo ya 12 ya  uvumbuzi wa teknolojia mpya ili kuongeza ushindani wa kiuchumi. Lakini nguzo nyingine pia ni muhimu. Kwa mfano miundombinu ya Marekani ikiwa ni pamoja na barabara na reli zinahitaji ukarabati mkubwa. Vilevile ubora wa elimu ya msingi na sekondari wa Marekani hasa katika shule za serikali katika maeneo ya watu masikini umeporomoka sana na unahitaji sera mwafaka ili ubora wa shule hizi ukaribie shule za nchi nyingine zilizoendelea.
Katika Taarifa ya WEF ya mwaka 2012/13, Rwanda imepanda nafasi 7  na kuwa ya 63 ukilinganisha na Taarifa ya mwaka 2011/12 ambapo ilikuwa ya 70. Rwanda inasifika kwa kuwa na asasi imara zinazozuia rushwa. Soko la ajira lina ufanisi na mnyumbuliko wa kutosha. Mabenki na soko la mitaji yameimarika na yanafanya kazi nzuri ya kukusanya akiba na kuwekeza vitega uchumi. Rwanda imewekeza kwenye TEHAMA na kuongeza kwa kiasi kikubwa utayari wake wa kiteknolojia. Kwa kuwa Rwanda haina bandari, ushindani wake wa kiuchumi unakwazwa na miundombinu ya nchi jirani ambako inalazimika kupitisha bidhaa zake.
Tanzania ilikuwa ya 120 katika Taarifa ya WEF ya mwaka 2011/12 na bado imebakia katika nafasi hiyo katika Ripoti ya 2012/13. Tanzania iko chini sana katika ushindani wa kiuchumi kwa sababu ya miundombinu mibovu. Tanzania ni ya 132 kati ya nchi 144 kwa ubora wa miundombinu. Tanzania bado iko chini katika elimu ya sekondari na elimu ya juu. Inashikilia nafasi ya 137 kati ya nchi 144. Tanzania pia iko chini sana katika utayari wa kupokea, kumudu na kutumia teknolojia na hasa matumizi ya mtandao wa internet ambapo inashikilia nafasi ya 122.
Ili Tanzania iweze kushindana na kunufaika katika ulimwengu wa utandawazi inahitaji iwekeze katika miundombinu ya barabara, reli, bandari, viwanja vya ndege, ufuaji na usambazaji wa umeme, miundombinu ya maji safi na maji taka TEHAMA na kuboresha elimu ya msingi, sekondari na vyuo vikuu. Ikiwa Rwanda imeweza kuongeza ushindani wake wa kiuchumi hakuna sababu kwa nini Tanzania ishindwe kufanya hivyo. Nchi inahitaji uongozi wenye dira, uadilifu na matumizi mazuri ya fedha za umma kuimarisha miundombinu na kuwekeza kwenye elimu bora ya vijana. Bila kuimarisha ushindani wa kiuchumi hatuwezi kuongeza ajira katika sekta za uchumi za kisasa.

No comments:

Post a Comment