Sunday, September 23, 2012

CHADEMA IMEDANDIA BEHEWA LA CUF!

Naibu katibu Mkuu JUVICF-Thomas Malima

Wengi tunaamini kuwa Elimu ni ufunguo wa maisha. Waandishi wamesomeshwa kwa kodi za watanzania kwa lengo la kupata elimu ya kuwahabarisha watanzania habari za ukweli na uhakika juu ya mustakabali wa maisha yao.

Lengo la elimu ni kujenga uwezo wa mambo makuu matatu kwa kila mwananchi ambayo ni uwezo wa kuhoji au kuuliza, uwezo wa kujifunza na uwezo wa kujiamini. Katika haya yote mkazo upo katika ubora na si vinginevyo, yaani kumjenga msomaji hasa mwandishi uwezo wa kufikiri, kusikiliza, kuuliza maswali, kupambanua na kuwasiliana na jamii bila kupotosha.

Baadhi ya waandishi wa habari nchini hawana uwezo uliotajwa hapo juu kutokana na kuandika makala zisizo na utafiti wala umakini kwa umma. Makala iliyoandikwa na mwandishi Mashaka Mgeta katika gazeti la Nipashe la tarehe 19 Septemba 2012 yenye kichwa CUF INAPOPANDIA BEHEWA LA CHADEMA ni ya kishabiki na yenye lengo la kuudanganya umma na zaidi ya yote imemdhalilisha mwandishi huyo pamoja na mhariri wa gazeti hilo kwa kuandika habari zisizo za utafiti.

CUF ilianza kauli mbiu yake ya VISION FOR CHANGE  mwaka 2008 na kuiweka rasmi kwenye Manifesto yake ya uchaguzi ya mwaka 2010. Tangu mwaka huo CUF haikuwahi kubadili kauli mbiu hiyo hadi wakati huu. Lakini cha kushangaza ni pale CHADEMA walipodandia kauli mbiu hiyo kwa kuzindua Movement for change M4C mwaka 2011. Ikumbukwe kuwa CUF iliinadi V4C nchi nzima wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2010 lakini leo baadhi ya waandishi wanajaribu  kuupotosha umma wa Watanzania kuwa CUF imedandia M4C ya CHADEMA. Je kwa ushahidi huo kati ya CUF na CDM nani amedandia hoja ya mwingine­­­­­?.

Hili si jambo la kwanza kwa CDM kuiga kutoka kwa CUF. Watanzania watakumbuka kuwa rangi za mwanzo za bendera ya CHADEMA  zilikuwa ni BLUE NA NYEUPE lakini baada ya kuona bendera za CUF zinavutia na zinaashiria mabadiliko ya kweli waliziiga na hatimaye kubadilisha bendera ya Chama chao ili zifanane na CUF kwa lengo la kuwatapeli wanachama na wafuasi wa CUF mikoani kuwa wao na CUF ni kitu kimoja hivyo wawape ushirikiano kwani wote ni wapinzani wa CCM.

CHADEMA pia waliendelea kuiga kauli  mbiu iliyokuwa inatumiwa na viongozi wa CUF kwenye mikutano yao. Watanzania watakumbuka kuwa  kaulimbiu ya mwanzo ya CHADEMA ilikuwa CHADEMA ……VEMA huku wakinyanyua vidole viwili. Lakini katika mkutano wa CUF kama chama kikuu cha upinzani kilichokuwa kinalea vyama vingine vidogo ikiwamo CHADEMA pale Viwanja vya BAKHRESSA mwaka 2004 ndipo aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar mheshimiwa Juma Duni alipozindua kauli mbiu ya NGUVU YA UMMA….CHACHU YA MABADILIKO. Baada ya mkutano huo ulioshirikisha vyama vingine kama CHADEMA ndipo Viongozi wa CHADEMA walipoamua kubadilisha kauli mbiu yake kuwa PEOPLES …..POWER. Iweje leo watu wasahaulishwe ukweli wa nani si mbunifu na nani anayesubiria mwingine abuni ili yeye aje na kukopi?.

Watanzania watakumbuka kuwa tangu CUF ilipoanzishwa ilikuwa na hoja ya Tanzania kuwa serikali 3 wakati CHADEMA ilikuwa inadai serikali ya MAJIMBO. Lakini cha kushangaza leo hii CHADEMA wamehama katika hoja yao ya Serikali ya majimbo na kuanza kuibaka hoja ya CUF ya serikali 3. Je hili nalo hamulioni kuwa CHADEMA hawana jipya bali wanasubiri CUF waibue hoja na wao ndo wanaibukia juu kwa juu?.

Suala mahitaji ya Katiba Mpya nalo limeonesha kuwa CUF ndicho chama pekee kilicho kinara cha Mabadiliko nchini maana CUF imesimamia suala hilo tangu kuasisiwa kwake hadi leo. WanaCUF walifikia hatua ya kufyatuliwa Risasi za Moto na kuwaangamiza zaidi ya wanaCUF 40 nchi nzima. Lakini leo juhudi hizo zinaelekea kupotezwa. Ni CUF pekee ndiyo ilikuwa na agenda ya Katiba mpya tangu 1995 lakini CDM imekuja kujitokeza 2010 tu. Je hapa pia hawakudandia hoja ya CUF ya Katiba mpya?.

Watanzania watakumbuka kuwa Mwenyekiti wa CUF alipotoka Marekani mwanzoni mwa mwaka huu aliwaeleza watanzania namna ambavyo rasilimali za nchi hii zikitumika vizuri zinaweza kuleta mabadiliko na kuwanufaisha watanzania. Profesa Lipumba alisema hayo baada ya kufanya utafiti kwa muda wa miezi 6 nchini Marekani , ambapo alipendekeza kuwaomba wapenzi na wanachama wa vyama vya siasa kuchangia vyama vyao ili vipate nguvu ya kifedha itakayoleta mabadiliko kwa kuingoa CCM. Baada ya kutoa hotuba hiyo,CHADEMA waliamua kufanya harambee ya kuchangia chama chao mwanzoni mwa mwezi juni 2012. Cha ajabu CUF waliofanyia utafiti uchangiaji huo, walipoamua kuweka katika vitendo juzi, wanaCHADEMA wameibuka na kusema CUF imewaiga. Je, kati ya CUF iliyotumia miezi 6 kutafiti na CHADEMA walioiga baada utafiti wa CUF nani amedandia hoja ya mwingine?.

Mwisho napenda kutoa wito kwa watanzania kutambua kuwa kila wanachokiona kinafanywa na CUF leo kimefanyiwa utafiti wa kina na kuthibitika kuwa kinafaa. CUF itaendelea kuwa baba wa ubunifu kwa vyama vyingine. CHADEMA wataendelea kuiga kutoka kwa CUF maana viongozi wake bado ni wababaishaji na wapiga domo tu.


Thomas D.C Malima
                         
  Mwandishi wa makala hii ni Naibu Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya vijana ya CUF-Chama cha Wananchi na anapatikana kwa simu namba 0715172256 na e-mail thommalima@yahoo.com.



No comments:

Post a Comment