TANZANIA INAHITAJI UONGOZI WENYE DIRA NA SERIKALI MADHUBUTI ILI KUJINASUA TOKA DIMBWI LA UMASKINI

Mwenyekiti Wa Cuf Taifa-Prof Ibrahim Lipumba
Nchi ambazo zimefanikiwa kukuza uchumi kwa kasi ya juu na kuwa na maendeleo kwa muda mrefu zimefanya hivyo kwa kuwa na uongozi adilifu, wenye dira na ulio imara katika uamuzi, utekelezaji na kujifunza toka kwenye makosa waliofanya na kujirekebisha.
 
Kuzungumzia uongozi na uadilifu katika siasa si jambo jepesi. Hisia na mitazamo ya watu wa kawaida kuhusiana na ‘siasa’ imekuwa ya kuihusisha fani hiyo na tamaa, ubinafsi, uroho, unafiki, ulaghai, upotovu, uovu, fitina, hiyana, na hata hujuma. Tena si watu wa kawaida tu bali hata baadhi ya wasomi wetu wanaonekana kuiona hivyo. Kwa wananchi wetu wa kawaida mtu akisifiwa kuwa huyo kwa siasa humuwezi, maana yake ni gwiji wa uongo na laghai. Hali hiyo kwa kiasi kikubwa imesababishwa na ubabaishaji wa uongozi wa kisiasa tuliokuwa nao na tunaoendelea kuwa nao.

Katika nchi masikini kama Tanzania, uongozi wa kisiasa ni muhimu katika kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa, kukuza na kupanua demokrasia na kuhakikisha kuwa nchi inaendeshwa kwa misingi ya utawala wa sheria, ambapo haki inatendeka na inaonekana inatendeka. Utawala wa sheria na haki sawa kwa wananchi wote ndio msingi imara wa amani na utulivu. Changamoto kubwa ya nchi yetu ni kujenga uchumi unaokua kwa kasi, kuongeza ajira na kuneemesha wananchi wote.

Tanzania inakabiliwa na changamoto mbili kubwa kujenga uchumi wenye manufaa kwa wananchi wote na kujenga demokrasia ya kweli itakayohakikisha nchi inaendeshwa kwa kufuata sheria zinazotoa haki sawa kwa wananchi wote. Nchi yetu inahitaji uongozi ambao unaona siasa ni utumishi wa dhati na uliotukuka kwa umma uliozindukana na siyo nyenzo ya kukimbilia na kupigania vyeo, fursa na nguvu ya ushawishi kwa malengo ya kujilimbikizia uwezo wa maamuzi na wa utajiri binafsi usiohojiwa.

Uongozi wa nchi unawajibika kubuni sera kwa kuzingatia uhalisia na hali ya uchumi wa nchi, fursa zilizopo na vikwazo vinavyoikabili nchi katika kukuza uchumi wake.  Baada ya kubuni sera uongozi unawajibika kuzieleza sera hizo kwa wananchi na kuwahamasisha waziunge mkono na waelewe kuwa ili kujinasua toka dimbwi la umaskini wanawajibika kuchapa kazi kwa bidii, kuweka akiba, kuwa wajasiriamali wabunifu na kukubali kasi ya mabadiliko inayoendana na ukuaji wa uchumi.  Uongozi utafanikiwa ikiwa sera zake zinaaminika na zinatekelezeka, na matunda ya sera hizo yanaleta neema kwa wananchi wote.

Uongozi makini utakaoweza kuchochea maendeleo ya muda mrefu unapaswa kuwa na subira, uwe na dira na mipango ya muda mrefu na ujikite katika lengo la kukuza uchumi utakaoongeza ajira na kuleta neema kwa wananchi wote. 

Katika zama za demokrasia ya vyama vingi ni muhimu kwa wadau vikiwemo Vyama Vya Siasa kukubaliana alau kwa ujumla dira ya maendeleo ya nchi na kila chama kitakachoingia madarakani kitekeleze sera zitakazokuza uchumi unaoleta tija na neema kwa wananchi wote.  Watendaji wazuri wa serikali walio waadilifu na uwezo mzuri wanasaidia sana katika kushauri wanasiasa walioko madarakani sera zinazotekelezeka na zenye manufaa kwa wananchi.

Baada ya muda mrefu bila ya kuwa na maendeleo ya kutosha, urekebishaji wa sera ni jambo muhimu.  Hata hivyo kurekebisha siyo lengo la mwisho.  Lengo ni matunda yanayotokana na kurekebisha sera hizo.  Nchi zilizofanikiwa kupata maendeleo ya muda mrefu, zimetegemea na kuutumia mfumo wa uchumi wa soko. Kuutegemea na kuutumia Uchumi wa soko hakumaanishi kuwa soko huria pekee ndiyo chanzo cha kukua uchumi.  Serikali madhubuti zilijenga mazingira ya kuwezesha sekta binafsi kutumia uchumi wa soko kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi.

Uchumi wa soko ulioendelea unajikita katika historia na asasi muhimu katika jamii husika.  Asasi hizo ni pamoja na kuwepo haki na uhuru wa kumiliki mali, mikataba, hususan katika shughuli za biashara na uchumi huheshimiwa na inapovunjwa kuna mamlaka zinazosuluhisha na kuhakikisha kuwa mikataba inasuluhishwa kwa gharama za wastani wa wale wenye haki wanapata fidia na hawadhulumiwi.  Taarifa kuhusu masoko zinawafikia wadau wote.

Katika hatua za awali za kutafuta na kuleta maendeleo, serikali makini zinafanya majaribio ya sera zake katika maeneo machache kabla ya utekelezaji katika nchi nzima.  Moja ya mapungufu makubwa katika kubuni na kutekeleza sera katika Tanzania ni ukosefu wa kufanya majaribio na kupima mafanikio yake kabla ya kutekeleza nchi nzima.  Matatizo haya yalikuwa makubwa wakati wa sera za ujamaa.  Kwa mfano sera za kuhamia vijiji vya kudumu kuwa ni amri mwaka 1974, Sera ya elimu kwa msingi kwa wote katika mwaka mmoja, sera ya kufunga maduka binafsi na kadhalika zilitekelezwa kabla ya kufanyiwa majaribio.  Hivi karibuni sera ya kuanzisha shule za sekondari za kata haikufanyiwa majaribio kabla ya kuitekeleza nchi nzima.  Ni muhimu katika utekelezaji wa sera, serikali ikafanya majaribio (pilot projects) na kujifunza katika majaribio hayo kabla ya kuitekeleza sera katika eneo kubwa.

Kubuni sera nzuri ni mwanzo tu.  Sera zinazopaswa kuwekwa katika mipango ya utekelezaji na kutekelezwa kwa umakini wa hali ya juu.  Utekelezaji na matokeo yake yafanyiwe tathmini ya mara kwa mara ili makosa yangunduliwe na kurekebishwa.  Kujenga utumishi bora, wenye ujuzi, usiyoyumbishwa na rushwa ndani ya serikali ni changamoto muhimu.  Utumishi mzuri ulio imara haujengwi siku moja.  Viongozi wa kisiasa ni wepesi kuhujumu kuwepo kwa utendaji mzuri serikalini ikiwa watawatumia watendaji wa serikali kufanikisha malengo ya kisiasa ya kubaki madarakani kwa kuiba kura wakati wa uchaguzi au utekelezaji wa miradi ya muda mfupi kwa malengo ya kuvutia wapiga kura.  Serikali inawajibika kuvutia watumishi wenye uwezo na ari ya kufanya kazi.  Ni muhimu mishahara ya wafanyakazi serikalini iwe inavutia lakini utunishi serikalini uzingatie uwezo na siyo mtoto wa nani au unamjua nani!

Serikali yenyewe siyo inayoleta ukuaji wa uchumi.  Kazi hiyo kwa sehemu kubwa ni ya sekta binafsi yenye wajasiriamali wazuri wanaowekeza na kutumia teknolojia bora na kuzitumia fursa zilizopo katika uchumi wa soko.  Hata hivyo serikali adilifu, yenye sera nzuri zinazojulikana na kutekelezwa kwa makini, isiyoyumba ni muhimu sana kwa maendeleo ya muda mrefu.  Kazi muhimu ya serikali ni pamoja na kuhakikisha kuna utulivu katika uchumi mpana kwa maana ya kutokuwepo mfumko wa bei kuwepo kwa akiba ya kutosha na fedha za kigeni kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nchi za nje, matumizi ya serikali na sekta ya umma yalingane na mapato ya serikali, na serikali iwekeze katika miundo mbinu muhimu.

Nchi zilizofanikiwa kukuza uchumi kwa muda mrefu zinafanya hivyo kwa kuwa na sera zinazoenda na mabadiliko ya uchumi ndani na nje ya nchi.  Mikakati ya kukuza uchumi ibadilike kufuatana na mabadiliko ya mfumo wa uchumi.  Siasa za ndani ya nchi pia zinastahiki kubadilika na kwenda na wakati.  Kukua kwa uchumi kutaongeza idadi ya watu wenye kipato cha kati na watu wenye elimu ambao watadai kushiriki katika maamuzi ya sera zinazowagusa na kuwa na sauti nchi yao.

Sera za kurekebisha uchumi ili kuchochea ukuaji wake na maeneo ya kuwekeza katika miundo mbinu ni mengi na yanazidi uwezo wa mapato ya serikali. Mkakati wa kukuza uchumi lazima uweke vipaumbele vya maeneo ambayo serikali itayashughulikia mwanzo.

Sera za kukuza uchumi endelevu zinajenga, mazingira mazuri ya uwekezaji mkubwa wa vitega uchumi, ongezeko la ajira, ushindani wa kibiashara, wepesi wa raslimali kutumiwa kwa shughuli mbadala (mobility of resources) hifadhi ya jamii na wananchi wote kufaidi matunda ya kukua kwa uchumi.

Hakuna nchi iliyofanikiwa kukuza uchumi kwa kasi ya juu kwa muda mrefu bila serikali kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika miundo mbinu – barabara, nishati, reli, bandari na mawasiliano, elimu na afya.  Uwekezaji wa serikali  katika sekta ya miundo mbinu, elimu na afya unajenga msingi imara unaovutia sekta binafsi kuwekeza katika shughuli za uzalishaji na biashara.  Uwekezaji wa sekta ya umma katika maeneo hayo unatengeneza njia yakuwezesha viwanda na makampuni mapya kuanzishwa na kuongeza faida ya shughuli zote za kibiashara zinazofaidika kwa kuwepo wafanyakazi wenye afya njema na walioelimika, kuwepo kwa barabara nzuri zinazopitika wakati wote, na kuwepo kwa umeme wa uhakika.

Nchini Tanzania, uwekezaji katika miundombinu umekuwa mdogo na hutegemea fedha za misaada toka nje.  Ukarabati wa miundo mbinu haufanyiki ipasavyo.  Barabara inajengwa inatumiwa mpaka inaharibika kabisa.  Ili ikarabatiwe tunaomba msaada kwa wafadhili waijenge upya.  Mifano ni Mingi.  Barabara ya Mandera, Barabara ya Dar es Salaam - Morogoro, Barabara ya Chalinze – Segera – Tanga, n.k

Ukuaji wa uchumi unaambatana na mabadiliko ya mfumo wa uchumi kutoka kutegemea sana kilimo na kuelekea kwenye ongezeko la ajira viwandani, kutoka nguvu kazi inayoishi vijijini kuelekea nguvu kazi inayoishi mijini.  Mabadiliko ya mfumo wa uchumi husababishwa na ushindani wa soko.  Serikali zenye malengo ya kukuza uchumi endelevu zinawajibika kujenga ushindani katika masoko yote kuruhusu makampuni mapya yenye tija kuanza na makampuni yanayopata hasara kufilisika.  Soko la ajira liwe jepesi kuruhusu makampuni mapya kuajiri wafanya kazi na makampuni yanayopata hasara kupunguza wafanyakazi.  Sheria za kazi zijikite katika kurahisisha uanzishwaji wa ajira. Ni muhimu sana kuwa na utaratibu wa hifadhi za jamii kwa wafanya kazi wanaopoteza ajira ili kupunguza makali na kuwepo kwa soko la ajira linalonyumbulika.  Wanaopoteza ajira wapate kipato cha kuwawezesha kuishi wakati wakitafuta ajira mpya.

Elimu bora inayowapa wafanyakazi uwezo wa kujifunza na kupata ujuzi mpya ni kinga muhimu ya kutopoteza ajira kwa muda mrefu.  Vile vile zinaongeza kasi ya ajira mpya kuanzishwa kwa wingi na kwa hiyo kuhakikisha nguvu kazi inaajiriwa. 

Mkakati wa kukuza uchumi lazima uzingatie kuwa toafuati kubwa za vipato vya wananchi kati ya maskini na matajiri havisaidii ukuaji wa uchumi na vinaongeza upinzani dhidi ya sera za kurekebisha uchumi.  Ni wazi uchumi unapoanza kukua tofauti za vipato zinaongezeka.  Sera zijikite katika kutoa fursa ya kupata ajira kwa wananchi wengi iwezekanavyo  na misaada maalum itolewe kwa watu maskini waweze kujinasua toka dimbwi la umaskini.  Vurugu za kisasa kupinga wachache kuwa matajiri wakati wengi ni maskini zitaathiri mikakati ya kukuza uchumi.

Kigezo muhimu cha kupima kama sera zinatoa fursa sawa kwa wote ni fursa za wasichana kupata elimu iliyo bora.  Wanawake walipata elimu, wanakuwa na watoto wachache wenye afya bora ambao wanawazaa wakati maungo yao yamekua.  Kina mama wenye elimu wanasisitiza na kuhakikisha kuwa watoto wao nao wanapata elimu.  Kuwaelimisha wasichana na kuwapa fursa ya kupata ajira ni nyenzo madhubuti ya kuutokomeza umaskini.

Nchi zilizofanikiwa kukuza uchumi kwa kasi zilitumia vizuri fursa zilizopo katika soko la dunia na kuongeza uuzaji wa bidhaa zao za viwandani katika soko hilo.  Sera za kuongeza uzalishaji wa bidhaa za viwanda hazikutegemea utaratibu wa soko huria tu.  Serikali zilijaribu sera mbali mbali za kutoa motisha wa kuongeza uzalishaji viwandani na kuuza bidhaa za viwandani nchi za nje.  Sera za kukuza sekta ya viwandani ni pamoja na ruzuku katika uzalishaji wa bidhaa mpya, uwekezaji wa miundo mbinu mizuri katika maeneo maalum ya kuanzisha viwanda vipya, misamaha ya kodi.  Ni muhimu motisha maalum kwenye viwanda vitakavyouza bidhaa nchi za nje zisiwe za kudumu.  Ikiwa sera hazikufanikiwa kuongeza kasi ya kukua kwa sekta ya viwanda na uuzaji wa bidhaa nchi za nje, sera hizo zibadilishwe.

Utandawazi umefanya uchumi wa dunia hivi sasa kuwa wazi zaidi na kuingiliana sana katika biashara, uwekezaji, huduma za fedha na teknolojia.  Nchi zilizokua kwa kasi ya juu zimefanya hivyo kwa kuingiza maarifa, teknolojia na ujuzi kutoka nchi za nje.  Njia moja ya kupata maarifa na teknolojia kutoka nje ni kupitia uwekezaji unaofanywa na makampuni ya nje.  Njia nyingine ni kupata elimu, maarifa na teknolojia iliyopo katika nchi zilizoendelea na kuitumia kwa kuzingatia uhalisi na mazingira ya nchi yako.

Uchumi wa dunia unatoa fursa ya soko kubwa kwa nchi zinazoendelea. Kinadharia, Tanzania inaweza  kuuza bidhaa zote za viwandani inazozalisha kwa bei ya soko la dunia. Suala la msingi ni je kuuza nchi za nje ndiyo njia pekee ya kukuza uchumi au tunaweza kukuza uchumi kwa kutegemea soko la ndani ya nchi?

Mikakati ya kuendeleza uchumi kwa kutumia soko la ndani inaweza kufanikiwa kwa muda mfupi hasa kwa nchi kubwa zenye watu wengi.  Zaidi ya hapo matatizo ya kutetereka uchumi yanaweza kutokea ikiwa nchi itafungua mipaka yake ghafla kwa bidhaa kutoka nje.  Hata hivyo mikakati ya uchumi inayotegemea soko la ndani tu hufikia ukomo wake mapema. Soko la ndani ni dogo mno kuendeleza ukuaji wa uchumi kwa muda mrefu na hautoi fursa ya kujikita na kubobea katika eneo la uzalishaji ambalo nchi ina ushindani au inaweza kujijengea ushindani mkubwa.

Ukuaji wa haraka wa uchumi katika nchi maskini hutegemea upatikanaji wa ajira kwa nguvu kazi ya ziada iliyomo nchini. Kwa kadri uchumi unavyokua ndivyo unavyoajiri nguvukazi ya ziada iliyomo nchini hasa vijijini katika sekta ya kilimo na iliyoko mijini katika sekta isiyo rasmi yenye tija ndogo.  Raslimali za nchi hasa nguvu kazi ni lazima ziwe tayari kuhama toka eneo au sekta yenye tija ndogo kwenda kwenye eneo na sekta zenye tija kubwa ambazo kwa kawaida huanzishwa mijini ambako ni rahisi kupata watu wengi wenye ujuzi na huduma muhimu kwa viwanda kama vile umeme na maji.  Ukuaji wa uchumi huambatana na ukuaji wa miji na nguvu kazi kuhamia mijini. Hata hivyo ili miji iwe vitovu vya ukuaji endelevu ya uchumi inahitaji miundombinu mizuri.

Sera za kukuza uchumi ni lazima zizingatie kuweko na utulivu katika uchumi mpana kama vile kuepukana na mfumko wa bei, ukosefu wa fedha za kigeni, ulimbikizaji mkubwa wa madeni ya sekta ya umma unaotokana na nakisi katika bajeti ya serikali na hasara za mashirika ya umma.  Vile vile mkakati wa uchumi unapaswa kutoa motisha kwa wajasiliamali, wadogo, wa kati na wakubwa kuwekeza katika sekta mbali mbali kwa kuwahakikishia kuwa wakifanya shughuli zao kwa ufanisi na kufanikiwa kupata faida, faida yao hiyo haitaporwa na vyombo vya dola au majambazi.  Vile vile ni muhimu kuwa na mikakati ya hifadhi ya jamii ya kupunguza makali ya maisha kwa watu watakao athirika na mabadiliko ya uchumi.

Kwa nchi zenye ziada ya nguvu kazi ukomo wa kasi ya kukua kwa uchumi unategemea kasi ya uwekezeshaji wa vitega uchumi.  Uwekezaji wa vitega uchumi hutegemea ukubwa wa akiba.  Ili uchumi ukue kwa kasi nchi inapaswa iweke akiba alau asilimia 25 – 30 ya pato la Taifa na kulimbikiza vizuri katika vitega uchumi vyenye tija kubwa.  Misaada kutoka nje haiwezi kuwa mbadala wa juhudi za kuweka akiba za ndani ya nchi za kila kaya, sekta binafsi na sekta ya umma ili akiba ilimbikizwe katika vitega uchumi muhimu.

Hivi sasa nchi yetu inakabiliwa na ombwe la uongozi na tumeshindwa kutumia raslimaliwatu na maliasili yetu kujenga uchumi unaoongeza ajira na kutokomeza umaskini. Nchi inahitaji uongozi utakaowaunganisha Watanzania kukabiliana na changamoto nilizozianisha katika mada hii. Watanzania tunapaswa kujiuliza bila kujali, itikadi, udini, ukabila na umajimbo nani katika viongozi wetu wa kisiasa wana dira na uwezo wa kuwaunganisha Watanzania kutekeleza dira ya mabadiliko itakayojenga uchumi imara, unaongeza ajira na kutokomeza umaskini? Tukiipoteza fursa ya kulijibu swali hili kwa vitendo mwaka 2015, tunaweza kujikuta tunapoteza miaka mingine 50 ya uhuru wetu bila kujiletea maendeleo na wananchi wengi kiendelea kubakia maskini wa kutupwa.


No comments:

Post a Comment